SAYYID MANSAB BIN ALI
Na Hamza Z. Rijal
Mwanachuoni aliyekuwa na Maajab
Alisoma mpaka uchoraji katika kanisa
Alikuwa akisoma sana majarida ya Misri
Alivutiwa sana Muhammad Abdoo wa Misri
Katika safu ya wanavyuoni wetu safari hii
tutamzungumzia Sayyid Ahmad bin Ali Itibar bin Mwinyi Mkuu Sultan Ahmad bin Ali
bin Abi Bakr bin Salim, zaidi akijulikana kwa jina la Sayyid Mansab bin Ali.
Sayyid Mansab alizaliwa Ukutani mwaka wa 1279 A.H
(1863), akiwa ametokana na mtoto wa kike wa Sayyid Ahmad bin Salim aliyekuwa
kadhi wa Sayyid Said.
Inafahamika kuwa Sayyid Mansab babu yake alikuwa ni
mfalme huko Ngazija. Wengi wa wafalme wa Ngazija walikuwa ni wa Ngazija wenyewe
kinyume na wafalme wa Zanzibar.
Babu yake Sayyid Mansab inasemekana alikuwa ni
mpenzi mkuu wa miti (ameature botanist) na mapenzi yake ya miti ilimuwezesha
kupeleka miti mingi ya vyakula nchini Ngazija, bwana huyu ananasibishwa na
Masharifu wote Moroni kutokana na asili yake, kama ilivyokuwa Masharifu wa
Jamalil-Leyl wanavyonasibishwa na Mwinyi Bahasani wa Tsujini.
Sayyid Mansab alianza kusoma elimu ya dini kwa
mjomba wake Sayyid Muhammad bin Ahmad bin Salim, na alielimika vya kutosha
kisha akasogea kwenda kupiga goti kwa Sheikh Ali bin Khamis. Sheikh Ali bin
Khamis siku hizo alikuwa akivuma sana kwa kukusanya elimu nyingi za dini, na
baada ya kutoka hapo Sayyid Mansaba alisogea kwa Sheikh Muhammad Al-Murony.
Kwa kuwa Sayyid Mansab alikuwa na sifa za kipekee
na mwenye kiu ya kukusanya elimu mbali mbali, hakusita hapo bali alikwenda
kujifunza uchoraji wa picha kwa bibi wa Kimisheni wa Kingereza kwenye kanisa la
Mkunazini, U.M.C.A (Kimoto).
Kwa kufanya hivyo Sayyid Mansab akapata pingamzi
kubwa kwa mashekhe wa siku hizo ambao walikuwa wakimpinga na kumuona mtu
asiyofahamika.
Vile vile alimfuata gwiji wa elimu ya tarekhe na
elimu ya fani nyenginezo mjuzi aliyekuwa akijulikna kwa jina la Hakim Daud Ali
Khan.
Hapo wengi ndipo walipozidi kumuona Sayyid Mansab
anakuwa na nadharia zisofahamika na kumuona kuwa atakuja kuleta athari kubwa
kwa vizazi vijavyo ikiwa haja dhibitiwa, na hayo yalikuja kuleta ithibati pale
alipokuwa akipenda kujisomea gazeti la "Manara" lililokuwa
likichapishwa nchini Misri. Sayyid Mansab alilipenda gazeti hilo kwa kuwa
lilikuwa na maudhui mengi ambayo yakipinga mambo ya uzushi ndani ya uislam, na
alikuwa ni mtu peke yake katika Unguja nzima akipokea gazeti hilo kwa njia ya
posta, tena zama hizo. Mwangalie Sheikh huyo alivyokwenda mbali na namna
alivyokuwa akipenda kuwa na uono mpana wa kielimu, ambao hata masheikh wetu wa
leo ambao wamefika vyuo vikuu mbali mbali hawana mtizamo wa aina hiyo.
Sayyid Mansab alikuwa akivutiwa sana na Muhammad
Abdoo mwanafunzi wa Jamaludini Afghani, na alikuwa akiitumia zaidi tafsiri ya
Sheikh Muhammad Abdoo na ikawa anavyosomesha yeye tafsiri ilikuwa ni tafauti
sana na masheikh wenzake na wale vijana waliokuwa wakisoma skuli za kizungu
wakihudhuria darasa zake walikuwa wakivutiwa mno kwani alikuwa akiweza kuelezea
ulimwengu kwa upana sana.
Hii ilitokana na kusoma magazeti mengi yaliyokuwa
yakitokea Misri, kama: Al-Hilal, Al-Muktatatf, Al-Liwaa, Al-Muayyad na mengi
mengine. Matokeo ya kupenda kuwa msomi wa fani mbali mbali yalitokana na
kupenda kukaa na wageni kama Sayyid Abdulrahman Jamal wa Misri, Sheikh Muhammad
Bakashmar, Sheikh Abdallah bin Salim Al-Khemry, Sheikh Muhammad Al-Izz na wengi
kama hao.
Mfalme wa nne katika wafalme wa Kibusaidy, Sayyid
Khalifa bin Said, mfalme huyu alikuwa hakubali kupigwa picha na alikuwa
hajawahi kupigwa picha, na Waingereza wakiheshimu jambo hilo, lakini Sayyid
Mansab alimpiga "drawing", kwa siri pasina mwenyewe kujua. Lakini
kama nilivyokwisha eleza kuwa masheikh wenzake walikuwa wakimpiga vita kwa
hivyo walifikisha habari kwa mfalme na Sayyid Mansab kuitwa na kuulizwa
"Kweli umeniandika sura yangu?" Sayyid Mansab akajibu na huku
anatetemeka "La, bwana wangu sithubutu".
Sayyid Khalifa akamwambia "Nikipata picha hiyo
utaona cha mtema kuni na ushuhudie kilichomtoa kanga manyoya, kwani
nitachokifanya nitakukata kichwa chako!". Na pale pale wakapelekwa watu
nyumbani kwa Sayyid Mansab kupekua, na kulipekuliwa kila mwahali kwenye nyumba
yake na hata mitungini kulimurikwa na kurunzi labda humo kuna chochote kile,
lakini kama waswahili wasemavyo "Wastara hazumbuki", alistirika
Sheikh na hakujapatikana chochote kile lau ingekuwa sio Sayyid Mansab picha ya
Sayyid Kahalifa isengekuwepo.
Ama wangeiona lazima Sayyid Khalifa angemkata
kichwa chake kama alivyosema. Sayyid Khalifa alikuwa hana mchezo atakalo ndilo
huwa., alikuwa akiwakata vichwa wahalifu kila siku ya Jumanne na Alkhamis.
Sayyid Mansab alikuwa khatibu wa msikiti wa Ijumaa
Forodhani kuanzia mwaka wa 1299 A.H (Septemba 1882) hadi 1337 A.H (Septemba
1919) alipomwachia mwanawe Sayyid Hamid. Alikuwa akisoma kwa kufuata kawaida
zote, kwa hivyo hata katika mashughuli mbali mbali akitangulizwa yeye kusoma.
Juu ya kupigwa vita na baadhi ya masheikh lakini
watu hao waliokuwa wakimpiga vita walikuwa wakielewa kuwa Sayyid Mansab alikuwa
gwiji, na iliposaliwa sala ya kuomba mvua wakati wa Sayyid Hamuud na zama za
Sayyid Khalifa bin Haroub alitangulizwa yeye kusalisha na hakuna aliyethubutu
kupinga hilo.
Sayyid Mansab alikuwa hatoki ila wakati maalumu,
wala haendi pahali ila mahali maalumu katika saa maalumu wala hafanyi jambo
maalumu ila katika muda maalumu pia. Alikuwa akiyafanya haya sio kwa kufuata
manazil ila alijiwekea taratibu hizo mwenyewe.
Sayyid Mansab alikuwa akitunza siha yake vilivyo na
yalikuwa maradhi ya kipuuzi hayamsogelei, lakini alipigwa na maradhi ya ghafla
yaliyodumu kwa masaa kumi na nne tu na ilipofika asubuhi ya Jumatatu mwezi 13
Mfungo saba mwaka wa 1346 A.H (10 Octoba 1927) akiwa metimiza miaka 67, Sheikh
alifunga macho na kuwachia watu pengo kubwa ambalo lilikaa kwa muda mrefu pasi
kuzibwa.
Ewe! Mola tupe nasi tuliopo hima kama aliyokuwa
nayo Sayyid Mansab na tufanikishe katika mambo ya kheri "AMIN".
(Maelezo haya nimeyapata kutokana na kitabu cha
Sheikh Abdallah Farsy "Baadhi ya Wanavyuoni wa Kishafi wa Mashariki ya
Afrika", na wazee wa Msikiti Gofu)
No comments:
Post a Comment