Sheikh Ahmad Bin Muhammad
Mlomry
Na Hamza Z. Rijal
Kati ya wanavyuoni wa Zanzibar
ambaye si haba alisafiri kwenda sehemu mbali mbali kufuata elimu sio mwengine
ila ni Sheikh Ahmad Bin Muhammad Mlomry.
Sheikh Ahmad Bin Muhammad Mlomry
inasemekana kuwa alizaliwa mwaka 1290 A.H (1873).
Sheikh Ahmad alianza
kusoma kwa Sheikh Ali Bin Abdallah Al-Mazrui na ndipo alipopata msingi wa elimu.
Baada ya hapo akaelekea Mombasa, na huko alikutana na wanavyuoni mbali mbali na
kukaa huko mpaka watu wakadhani kuwa hatorudi tena Zanzibar.
Alirudi Zanzibar
baada ya kufa Sheikh Ali bin Abdallah. Kabla hajenda kusoma kwa Seyyid Ahmad
bin Sumeyt na Sheikh Abdallah Bakathir, alikwenda kusoma kwa Sheikh Muhammad
bin Ahmad Al-Muroni na kwa Sheikh Abdul-rahman Mweze Mbamba.
Sheikh Ahmad Bin
Muhammad Mlomry alikuwa kati ya wanafunzi wakubwa wa Sayyid Ahmad bin Sumeyt na
Sheikh Abdallah Bakathir, na akawa mwenye kuhudhuria darsa zao zote walizokuwa
wakisomesha na akawa ni mwanafunzi aliyekubalika na Alim wote hao wawili
walikuwa wakimtukuza na walimkubali ya kuwa anafahamu vizuri.
Kwa hivyo wakiulizana
nae katika baadhi ya mambo yanayofanya matata na wengi wakisema Sheikh Ahmad
amepata kufunuliwa elimu na wajuzi hawa wawili.
Hapo mwanzo
nilikwishaeleza kuwa Sheikh Ahmad akipenda kusafiri kwa kwenda kutafuta elimu
na katika safari zake alitembelea nchi ya Misri, Sham na nchi nyenginezo.
Kati ya aliobahatika
kukutana nao Misri alikuwa ni Sheikh Muhammad Abdoo. Huyu alikuwa ni Mufti wa
Misri nzima na ni mwanachuoni mkubwa kabisa. Sheikh Ahmad aliweza kudondoa cha
hapa na pale kwa Mufti huyo, kisha akahudhuria darsa za Sheikh Salmy Al-Bishry,
Sheikh Al-Islam wa Misri na vile vile akaenda kwa Seyyid Ahmad Bey-Al-Husseyny,
huyu akiwa ndio mtu wa mwanzo kupiga chapa ‘Al-Umm’ ya Imam Shafi, akampa hiyo
Al-Umm na vitabu vyengine Sheikh Ahmad ili iwe hidaya kwake.
Na alipofika Hijaz
kati ya aliyekutana nao alikuwemo Sheikh Muhammad Bin Suleiman Hasballah. Huyu
ni mtunzi wa kitabu “Riyadhal-Badiah”, na Sheikh Ahmad alimtaka mtunzi huyo
ampe ‘Ijaza’ ya kusomesha kitabu hiki na vyenginevyo, naye alimpatia Ijaza.
Naye Sheikh Ahmad alivisomesha vitabu hivyo vyote na kuwapa baadhi ya wanafunzi
wake Ijaza.
Katika
usomeshaji wa darsa, Sheikh Ahmad alikuwa akisomesha kwake nyakati za usiku na
akisomesha nyakati za alasiri na zile nyakati za asubuhi akipatikana Msikiti
Barza na katika mwezi mtukufu wa Ramadhani alikuwa na kazi nzito ya kusomesha
kwani alikuwa akidarasisha kuanzia saa 5 asubuhi hadi nyakati za alasiri.
Baada ya kustakimu
siku nyingi Zanzibar, Sheikh Ahmad alihamia Ngazija na huko alikuwa na
wanafunzi wengi, lakini inavyoeleweka Sheikh Ahmad hajaishi siku nyingi nchini
Ngazija na alifia mji wa Mitsamihuli Mwezi 23 Mfunguo 7 mwaka 1357 A.H (23 Juni
1936).
Sheikh Ahmad Bin
Muhammad Mlomry ni mtu wa kupigiwa mfano kwa safari zake za nje za kwenda
kutafuta elimu na kubahatika vile vile kukutana na vigogo mbali mbali, ambavyo
vilimmiminia elimu si haba.
Mola atupe hima nasi
kuuiga mfano mzuri wa Sheikh Ahmad Bin Muhammad Mlomry
“Ameen.”
No comments:
Post a Comment