Sheikh Muhyiddin Bin Sheikh
Na Hamza Z. Rijal
Kati ya maalim wa Kishafi waliotia msingi wa elimu ya dini
Visiwani ni watatu, nao ni: Sheikh Muhyiddin, Sheikh
Ahmed Bin Sumeyt na Sheikh Abdul-Aziz Bin
Abdul-Ghany Al-Amawy.
Sheikh Muhyiddin Bin Sheikh alizaliwa Barawa mwaka wa 1206
AH(1718 AD). Katika zama zake katika uwanja wa elimu ya dini ya kiislam,
ilikuwa huwezi kutaja wasomi wa kiislam wawili asiwe yeye ni mmoja.
Makaazi yake yalikuwa ni Mombasa wakati wa zama za Sayyid
Said, wengine wanasema kuwa Sheikh Muhyiddin kuja kwake Zanzibar kulitokana na
kutakiwa kufanya hivyo na Mfalme Seyyid Said.
Alitokea kupendwa sana na Mfalme huyo na alikuwa akipelekwa
nchi mbali mbali zilizokuwemo chini ya himaya ya Ufalme, akafanya suluhu pale
panapotokea mtafaruku na mara nyingi alifaulu kutekeleza kazi hiyo.
Sheikh Muhyiddin ndiye mjenzi wa Msikiti wa Ijumaa wa
Malindi, ambao hivi sasa umejengwa tena kwa kufuatwa kigezo kile kile cha
mwanzo.
Sayyid Majid Bin Said Sultan alimsaidia sana katika ujenzi
wa Msikiti huo. Baada ya ujenzi wa Msikiti huo, Sheikh Muhyiddin alijisogeza
Msikiti wa Kiponda uliokuwa karibu na Sharif Dewji, lakini kwa siku hizi
tutaita kwa Makapu.
Sheikh Muhyiddin alisomesha wanafunzi wengi, ambao baadae
walikuja kuwa ni walimu wakubwa kabisa, kati ya hao ni Sayyid Ahmad Bin Salim
Bin Abubakar Salim, Sheikh Abdul-Aziz Bin Abdul-Ghany Al- Amawy, Sheikh
Suleiman Hayat, Sheikh Muhammed bin Ahmed Bin Hassan Al-Murony, Sheikh Hassan
Bin Yussuf Mugazija, Sayyid Omar Bin Salim Baalawy, Sheikh Ahmad Bin Salmin
As-Sabahy, Sheikh Fadhil Bin Ali Mugazija, na Sheikh Shauri Bin Haji Shirazy.
(Toleo litalofuata nitawazungumza hawa wote kwa Mukhtasar, yaani wanafunzi wa
Sheikh Muhyiddin.)
Katika sifa nzuri alizokuwa nazo Sheikh Muhyiddin, ni
alikuwa mtu mwenye uadilifu. Hukumu zake zote zilikuwa hazina upendeleo, ilitokea
safari moja Sayyid Bakarish Shatry alikuwa na kesi yake na mwenziwe, basi
akenda kwa Sheikh Muhyiddin akampa riali 50, Sheikh Muhyiddin alipomuuliza za
nini? Sayyid Bakarish akamwambia hiyo ni zawadi tu, hiyo ni tunu. Sheikh
Muhyiddin akapokea akenda nazo ndani akazifunga vizuri, zote pamoja na roboto
moja, akaandika juu ya roboto "Hii dhamana ya Sayyid Bakarish Shatry,
nikifa apelekewe mwenyewe", basi alipokufa agizo lake lilitekelezwa.
Angalia insafu ya watu waliokuwa nayo ya mtoaji wasia na watekelezaji wa wasia.
Sheikh Muhyiddin alitunga vitabu vingi kati ya hivyo ni:
- Kitabu kidogo cha Tawhid,
- Mashairi ya Kiarabu,
- Mashairi ya Kiswahili,
- Tarehe ya Kilwa (Sulwa fy Akhbar Kulwa),
- Utenzi wa Hadithi ya Miraji,
- Kitabu kidogo cha kufundishia Sarfu na
- Sherhe ndogo ya Khutba ya Minhaj.
Vile vile
aliandika shairi la dua ya kuomba mvua katika mwaka 1278 AH (1862)
Hebu na tuzisome beti saba za shairi hilo.
1.
Naanza kubtadi, Kwa isimu yake Karima
Kuomba
Wadudi, Mtukufu mwenye adhama
Nabii
Muhammadi, Msalie kiumbe chema
Tupate miradi, Ifurahi yetu
mitima(nyoyo)
Siku
ya tanadi(kiama), Waja asi wakilalama
2.
Na alize thama(kadhalika), Watukufu wenye ajiri(thawabu)
Wenye
sifa njema, Simba zake tumwa bashiri
Na
waliosimama, Kuendesha mambo ya kheri
Hao
wa qadima(zamani), Na nyengine zote dahari
Siku
ya qiyama, Tuokoke na Jahannama
3.
Nimetia tama(nimemaliza), Dibaji sitakithiri
Nina
mambo mema, Nayawaza kiyafikiri
Haya
makulima, Yadhiika kwa nyingi hari
Twaomba
rehema, Kwa Wahabu mwenye amri
Tutuze
mitima, Kwa rehema yako Karima
4.
Mola Subhana, Mola wetu uso shirika
Ndiwe
Rahmana, Na Rahima uso shaka
Warehemu
wana, Na wazee wenye mashaka
Waijua
sana, Hali yetu kati ya chaka(kukosa mvua)
Jua la mchana, Na usiku lisilokoma
5.
Ilete mvua, Iondoke nyota(kiu) na jua
Ndiwe
mwenye quwa(nguvu), Ufishao na kufufua
Hali
waijua, Huhitaji kuarifiwa
Hasha
kuemewa, Ni amri ‘KUN’ ikawa
Wala kutendewa, Jalla Rabbi mwenye
adhama
6. Wengi waaayisi(wamekata tamaa),
Kwa mateso kuwa tawili
Wana
wasi wasi, Kwa madhambi yao thaqili
Rabbi
tunafisi, Mola wetu uso mithali
Na
yawe mepesi, Iwe ‘KUN’ yako kakima
7.
Rabbi twafikie, Toba njema yenye nadama(majuto)
Utughufurie,
Kuu dhambi ziwe lamama(ndogo)
Wewe unenee, ‘Ud-uni’ yako kalima
Tuwasalie, Kwa isimu yako adhima
Dua na ipae, Na qabuli ije kwa hima.
Sheikh Muhyiddin alifariki katika mwezi wa Shaaban tarehe 27
mwaka 1286 AH (Disemba 1869). Akiwa ameacha pengo kubwa baada ya kuaga dunia,
lakini si haba kwani aliacha wanafunzi wengi ambao walikuwa wakisifika na
kuifanya kazi aliyoiacha Sheikh wao barabara.
"Ewe Mola tupe hima na juhudi za watangulizi wetu hawa
waliopita Ameen,"
No comments:
Post a Comment