Wednesday, 1 April 2015

Sheikh Shauri Al-Shirazy - Hamza Z. Rijal


Sheikh Shauri Al-Shirazy
Na Hamza Z. Rijal
Zanzibar ilikuwa ni kituo muhimu cha elimu ya dini ya kiislamu hata pale waislamu wa Afrika Kusini walipotanzwa juu ya suala zito la kidini na kukosa wakulisuluhisha suala hilo, ndipo walipoamua kulipeleka suala hilo Makka ili kuweza kupatiwa ufafanuzi. Maulamaa wa Makka waliipa kazi hiyo maulamaa wa Zanzibar.

Zanzibar ilikuwa ni kioo kwa yule atakayekujitizama uwezo wake kielimu, hayo yalishamiri katika kipindi cha karne ya 19 hadi katikati ya karne ya 20.

Walipita masheikh wakubwa wakubwa ambao wakitukuzwa kwa elimu, adabu na mwenendo mzuri waliokuwa nao. Miongoni mwa wanavyuoni waliokuwa maarufu zama hizo na kuacha athari kubwa baada ya kuondoka kwao, mmoja wao alikuwa ni sheikh Shauri Bin Haji Ashirazy mzaliwa wa Tumbatu.

Sheikh Shauri inelezwa kuwa alisoma kwa gwiji ambaye alikusanya fani zote za elimu ya dini ya kiislamu ambae ni Sheikh Muhidin bin Sheikh. Kati ya wanafunzi ambao Sheikh Shauri alipiga goti nao kwa Sheikh Muhidini, walikuwa Sayyid Ahmed bin Salim , Sheikh Abdul Aziz bin Abdul Ghany. Sheikh Suleiman Hayat na wengineo .

Aidha inaelezwa kuwa Sheikh Shauri bin Haji alipokuwa katika umri wa makamo aliondoka Tumbatu na kuelekea mjini kuitafuta elimu kama tunavyosisitizwa na dini yetu ya kiislamu kuwa tuitafute elimu popote pale kama hadithi ya bwana mtume isemavyo: "Itafteni elimu hata China".

Kama nilivyotangulia kueleza kabla, kuwa mwalimu wa sheikh Shauri alikuwa ni Sheikh Muhidin Bin Abdallah Al-Kahtany, Sheikh Shauri alifika pahala ndipo kwa kujiendeleza na kujikuza , kwani Sheikh Muhidin alikuwa na uwezo wa kutoa fatwa mas-ala mbali mbali ya kidini na akisomesha fani mbali mbali za elimu ya dini. Ilikuwa kupita kwake na kuambiwa umekubalika ilikuwa ni sawa kwa sasa umefuzu katika chuo kikuu chochote kile cha kidini.

Kutokana na kazi zake Sheikh Muhidin kuzimudu vya kutosha ndipo hata mfalme wa siku hizo Sayyid Said alivutiwa naye na kumpa kazi ya ukadhi. Sheikh huyu inafahamika kuwa ndiye aliyejenga msikiti wa Ijumaa wa Forodhani kwa kusaidiwa na mfalme wa wakati huo Seyyid Majid Bin Said bin Sultani.

Baada ya Sheikh Shauri kuhitimu masomo yake na kukubalika kuwa sasa anaweza kudarasisha, Sheikh Muhydin alimpa ruhusa mwanafunzi wake arudi shamba, lakini safari hii badala ya kurudia Tumbatu alitua Donge. Maskani yake ya kwanza ilikuwa ni Donge Muwanda, hapo aliweza kujinunlia shamba na kustakimu. Aliweka darsa kubwa ikawa watu wanatoka maeneo mbali mbali kwenda kusoma kwake na wengi wa wanafunzi walikuwa wanatoka Kinyasini, Bumbwini na umbali wa kutokea Tumbatu. Wote hao walikuwa wakifuatia darsa za sheikh huyu mashuhuri.

Mbali ya darsa za kila siku, vile vile Sheikh Shauri alikuwa akiendesha darsa za wiki. Inaelezwa kuwa sheikh huyu akiimudu vilivyo darsa ya kutafsiri Qurani kwa kutumia kitabu cha “Jalaleyn”.

Mbali ya tafsiri ya Qurani aliyokuwa akisomesha vile vile vitabu alivyokuwa akidarasisha vilikuwa pamoja na Taajul Arusi cha Sheikh Sakandri, Ulbati Sadik , Murshadi Awami, Ghaya na vyenginevyo ambao warithi wake wote nao walikuwa wakivisomesha na vinaendelea kusomeshwa hadi hii leo.

Baada ya Sheikh Shauri kuona kazi yake imeweza kutoa matunda alihamia Donge Msalani, kama alivyofanya alipokuwa Donge Muwanda na hapo Donge Msalani alijinunulia shamba ambalo ndilo lililokuwa likimuendesha maisha yake. Watu wa daraja za kina sheikh Shauri ni kati ya wale walioufahamu fika mwenendo wa Mtume Muhammad (S.A.W) wa mtu kupata riziki yake kwa jasho lake kinyume cha wale tuliokuwa nao zama hizi.

Aidha historia inaeleza kuwa Donge Panga Maua ndio kilikuwa ni kituo cha mwisho cha Sheikh Shauri. Inafahamika kuwa sheikh Shauri aliweka markaz kubwa hapo Donge Panga Maua na alipata wanafunzi wengi ambao baadaye walishika makamo yake. Kati ya hao ni Sheikh Haji Bin Vuai Shirazy na Sheikh Suleiman Ali. Hawa wawili walikuwa ni wazaliwa wa Donge , vile vile sheikh Ali bin Umar Shirazy huyu alikuwa kati ya wanafunzi wake wakubwa ambaye hakuwa mkazi wa Donge.

Mbali na kuwafunza wanaume , aliweza kumuelimisha vya kutosha mkewe Mwana Alama ambaye naye alikuwa akidarasisha wanawake wenzake na kuendeleza darasa kwa wanawake. Ilikuwa kwa mwanamke haina haja ya kwenda kuuliza kwa Sheikh kwani bibi huyu naye alikuwa akizimudu fani nyingi, ambapo kwa hivi sasa wanakosekana wanawake wa sampuli hiyo.

Sheikh Shauri alibarikiwa watoto watano akiwemo Shadhili, Moh’d, Mahmond na wawili wakiwa wasichana. Shadhili Shauri Shirazi ni mmoja kati ya watoto wake ambaye alifanikiwa uzazi na kuzaa watoto saba akiwemo Haroun, Daud,Farasini, Shauri, Abdulsamad, Ziyabu na Khadija.
Kwa mujibu wa simulizi za uhakika Sheikh Shauri Shadhili Shauri al Shirazy wengi wakipenda kumwita Shauri mdogo, kijana huyu aliweza kuelimika vya kutosha kutoka kwa baba yake Sheikh Shadhili, na ndipo ukasibu ule msemo mtoto hufuata kisogo cha mzeee wake. Shauri mdogo alishika usukani naye baadaye akaziendeleza darsa alizozirithi kwa baba yake ambaye zinatokana na msingi aliouweka babu yake.

Ni jitihada ya kushukuriwa ya kina sheikh Machano na sheikh Shamim ya kuendeleza elimu katika eneo la Donge ambayo mwanzilishi wake ni Sheikh Shauri. Pamoja na masheikh hawa wawili kuwa na shughuli nyingi mjini, hawakuitupa Donge na kukumbuka kuwa mtu kwao ugeni sio kitu chema. Masheikh hawa hutumia siku za mwisho wa wiki kwenda Donge na kudarasisha.

Leo Donge zipo darsa, lakini sio kama zilivyokuwa zikiendeshwa siku za Sheikh Shauri mwenyewe, jitihada zaidi zatakikana kwa upande wa masheikh na wanafunzi kwa kuweka misingi madhubuti ya kuihuisha dini yetu na kuirejeshea Donge hadhi yake na Zanzibar kwa jumla.
Tunamuomba “Allah” atuwafikishie hayo. “AMIN” 

No comments: