Baadhi ya Masheikh Waliopita Zanzibar
na Kuweka Msingi wa Elimu ya Dini ya Kiislamu
Sheikh Muhammad Bin Umar Al-Khatibu
Na Hamza Z. Rijal
Katika mfululizo wa
makala za wanavyuoni wetu hii leo tutamuangalia alimu mwengine wa visiwani humu
kwa jina ni Sheikh Muhammad Bin Umar Al-Khatibu.
Sheikh Muahammad Bin
Umar kama watu walivyopenda kumwita bwana wa Shangani/Shakani, alizaliwa mwaka
wa 1239 A.H (1876). Unapojaribu kutaka kumzungumza Sheikh inakubidi kwanza
umtizame ni nani mwalimu wake? Katika wanafunzi wengi wa Sheikh Abdallah
Bakathir (1860-1925) aliowasomesha pale alipokuwa keshastakimu Unguja alikuwa
ni Sheikh Muhammad Bin Umar.
Sheikh Muhammad Bin
Umar alipelekwa kupiga goti na kupinda shingo (kusoma) kwa Sheikh Abdallah
Bakathir na hapo aliweza kuonyesha jitihada kubwa ya kujifunza, na Sheikh
Bakathir akatokea kumpenda mno na kumfanya kati ya watu wa aila yake na alikuwa
akiandamana naye popote pale alipokuwa anakwenda na Sheikh anahakikisha kuwa
Sheikh Muhammad Bin Umar yupo naye popote pale aendapo.
Sheikh Muhammad Bin
Umar alipokuwa anajifunza na wanafunzi wenzake ikiwa wa makamo yake na wengine
waliomzidi hirimu, kilimchukua kipindi cha muda mfupi sana kutokana kuwa
mwanafunzi hodari na aliweza kuwa taliisha wenziwe na muda usio mrefu, aidha
alipata makamo ya kusomesha darasa ndogo ndogo hapo Ukutani.
Ukutani katika
nyakati hizo ilikuwa ni sawa na "College’ yeyote ile kubwa ya kidini hivi
sasa duniani, kwani wanavyuoni takriban asilimia kubwa walipitia hapo na
kusomesha Ukutani na wasomi hao walikuja kukubalika nje ya Afrika Mashariki
ikiwemo Hadharmout, Makka na Misri.
Sheikh Muhammad Bin
Umar inasemekana kuwa alikuwa na wake wawili, mmoja akikaa mjini na wa pili
akiishi naye katika mtaa wa kikwajuni ambako alikuawa akidarasisha baadhi ya
siku za wiki katika Msikiti wa Kikwajuni ukijulikana kwa saa Msikiti wa
Ahli-Sunna.
Kilimchukua kipindi
kifupi cha kusomesha watu wa hirimu yake ambacho kilidumu miaka saba kabla ya
kupewa makamo kamili ya kudarasisha darasa zote alikuwa akianza kudarasisha
mara tu baada ya sala ya alfajiri, hadi saa tano za asubuhi, wanafunzi
wakibadilishana kwa makundi.
Kundi hili likimaliza
kundi jengine linaingia, na hivi ndivyo walivyokuwa wakisoma watu na namna
walivyokuwa wakisomesha. Na wengi wa wanavyuoni wetu walipitia mkondo huu
kusoma na kutalii na wenzao kuanzia asubuhi hadi Isha.
Suala la kujiuliza ni vipi wakijiendesha kimaisha?
Kila mmoja alikuwa na sampuli yake, wengine walikuwa wametolewa makwao na kila
haja zao zilikuwa zikikidhiwa makwao, wengine walikuwa na mali za kurithi
nyumbani, wengine walikuwa wafanya biashara, na wengineo hawajakuwa na lolote
ila wakijifunza na kuangalia bahari ya maisha itawachukua vipi na kuwaweka
wapi.
Msikiti Gofu ni kati ya misikiti michache visiwani
humu kuwa wanasali sala ya Tarawehe na Sala za witri kwa mtindo wa kusomwa
juzuu kamili, jema linaloendelea hivi sasa ni misikiti isiopungua 20 hivi
visiwani inakwenda na mtindo wa kusali Tarawehe na Witri kwa usomaji wa juzuu
nzima. Msikiti wa pili kusali Tarawehe na Witri kwa kusoma Juzz nzima ulikuwa
Msikiti wa Chwaka katika Karne ya 19.
Sheikh Muhammad Bin Umar alipewa makamo ya kusalisha Tarawehe
na Witri wakati walimu wake wakuu wa hai na wakiwa nao wakihudhuria sala hizo,
hao sio wengine ila ni Sheikh Abdallah Bakathir na Sayid Ahmed Bin Sumeit.
Sheikh Muhammad Bin Umar alidumu kuzisalisha sala hizi
hadi pale alipokuja kupokewa na Sheikh Abdallah Bin Farsy katika mwaka wa 1933.
Sheikh Muhammad alikuwa akiisoma Quran kwa hukmu zake
na kwa ukamilifu, jambo ambalo lilimfanya achaguliwe kuwa Khatibu wa Msikiti
Ijumaa wa Malindi na Sheikh Abdallah Saleh Farsy anatueleza kuwa
"hakutokea Khatibu katika Unguja, Pemba, Mrima, Mombasa na Lamu mwenye
sauti ya juu na kali kama Sheikh Muhammad Bin Umar."
Sheikh Muhammad Bin Umar alidumu kusomesha Msikiti wa
Kikwajuni, na alihamia Msikiti Gofu kusomesha darasa zake zote katika mwaka wa
1927 alipokufa Sheikh Muhammad Bin Abdallah Al-Hinzwany.
Alikuwa na darsa nyingi akizisomesha hapo Msikiti Gofu
na alizidi kutwikwa mzigo na mzigo kumuelemea pale Sheikh Muhsin Barwany
aliposhindwa kuzisomesha darsa pale Ukutani kuzidiwa na maradhi na kupokewa na
Sheikh Abubakar, na mwisho Sheikh Muhammed Bin Umar akaendeleza darsa na watu
wakawa wanajihisi kuwa zimeondoka sura tu za watangulizi wake lakini taaluma
waliokuwa wakiipata ni ile ile.
Darsa zake zilikuwa zikihudhuriwa na watu ambao
walikuwa wa madhehebu nyenginezo, lakini waliyaweka madhehebu upande na kwenda
kuchota elimu kwake, kwani alikuwa ni kisima chenye kina kirefu na maji yake
yapo saa zote na kila yakitekwa basi huzidi kuja juu.
Alipokufa Sheikh Abubakar alikuwa yeye ndiye mwenye
amri zote za nyumba mbili za Ukutani kwani, bwana huyu alipata bahati nzuri ya
kumuoa mtoto wa Sheikh wake, kwa hivi ni kusema kuwa Sheikh Abdalla alikuwa
mkwewe na Sheikh Abubakar na ndugu zake wanakuwa shemegi zake, ni Sheikh
Muhammad Bin Umar aliyetoa shauri ya kufanya nyumba mbili za ukutani kuwa ni
nyumba za wakfu na kila mmoja wao akaridhia (soma makala ifuatayo juu ya
tarekhe ya Ukutani).
Wengi wa Masheikh waliopita walikuwa na muandiko
mzuri, naye Sheikh Muhammad Bin Umar alikuwa na muandiko wenye kupendeza
kuusoma na yeye ndiye aliyeandika "Muswada" (Manuscript" wa
baadhi ya vitabu alivyovitunga Sayyid Ahmad na Sheikh Abdalla; na kavisoma
mbele yao, na wao wakamsikiliza).
Sheikh Muhammad Bin Umar alifunga macho usiku wa
kuamkia Jumaane tarehe 30 Mfunguo Tisa 1377 A.H (21.1.57).
Msikiti Gofu na Ukutani kama nilivyokwishaeleza
wanavyuoni tele wakisomesha hapo na kusomea hapo, na mwahali humu mulikuwa ndio
chimbuko la elimu hapa visiwani, Leo Msikiti Gofu darsa ya pekee iliyo na
wanafuzni wengi ni ile ya mwezi wa Ramadhani baada ya sala ya Alasiri ya
tafsiri ya Quraan isomeshwao na Mufti Sheikh Harith Bin Khelef, lakini Gofu
haina tena darasa nzito nzito zilizopata kuweko ingawa kuna darsa ndogo ndogo
tu, na Ukutani nayo imepoteza mkondo wa taaluma iliyopata kuweko ingawa elimu
bado inasomeshwa.
Wako wapi watakaochukua jukumu la kuirejesha hadhi na
mkondo wake uliopata kuweko mwahali humo mwenye historia kubwa ya elimu ya dini
visiwani, yaani Msikiti Gofu na Ukutani.
Tunamuomba "Allah" azirejeshee Unguja na
Pemba yake elimu ya Kiislam kama walivyokuwa nayo kina Sheikh Muhammad Bin Umar
na wengineo "Ameen. ’’
No comments:
Post a Comment