Monday, 31 August 2015

KISA CHA ZAHAKI RASHID: KUTOKA MAUAJI YA MWEMBECHAI 1998 HADI MAUAJI YA STAKISHARI 2015


Zahaki Rashidi


Ndugu msomaji,

Ili uweze kufaidikia na kisa cha Zahaki Rashid ni muhimu kwanza usome mwanzo wa matatizo yake mwaka wa 1998 baada ya kutokea mauaji ya Mwembechai yeye akiwa afisa wa polisi.

Tafadhali ingia hapa: 
Zahaki, mtuhumiwa wa Stakishari anayeamini anafanyiwa visasi
-        Alikuwa shuhuda muhimu wa Mauaji ya Mwembechai
Zahaki Rashidi Ngai si jina geni katika masikio ya Waislamu wengi hapa nchini. Yeye ni mmoja kati ya wanaharakati wachache ambao wametajwa sana  na masheikh, vyombo vya habari na hata katika vitabu maarufu vilivyoandikwa na waataaluma wa Kiislamu.
Umaarufu wa Zahaki umetokana na kutajwa  shuhuda muhimu wa tukio la mauaji ya Mwembe Chai na dhuluma mbalimbali ambazo Serikali imewatendea Waislamu.
Kwa mara ya kwanza, Zahaki alitoa ushuhuda wake kwa mwanahistoria maarufu Muhammedi Saidi. Alifanyiwa mahojiano maalum kuhusu ukweli wa mauaji ya Mwembe Chai. Hapo aliyasema yote aliyoyaiona na aliyoyaamini.
Baada ya hapo, ushuhuda huo ulichapishwa katika kitabu maarufu cha Prof. Hamza Njozi, kilichoitwa, ‘Muslim and state in Tanzania’ .
 Zahaki atajwa katika ujambazi  
Akizungumza na gazeti la Imaan kabla ya kwenda polisi kuhoji kutajwa kwa jina lake katika taarifa zilizozagaa katika mitandao ya kijamii akitajwa kama miongoni mwa wahumiwa wa mauaji yaliyotokea  kituo cha polisi Stakishari.
Alisema baada ya kupokea taarifa hizo za kuhusishwa na uhalifu huo, hatua ya kwanza aliyofanya ni kutaka kukutana na waandishi wa habari ili Waislamu wenzake wajue ukweli juu ya dhuluma ambayo jeshi la polisi linajaribu kumfanyia akiamini inatokana na historia yake ya kusema kweli kuhusu tukio la mauaji ya Mwembe Chai.
Alisema kinachotokea sasa ni matokeo ya chuki na kisasi cha muda mrefu kilichotokana na uamuzi wake ya kusema kweli katika tukio lile la mwaka 1998 ambalo lilipelekea kufukuzwa kazi ya polisi na kufedheheshwa baada ya kulikosoa jeshi hilo.
“Najua mtuhumiwa akishafika katika mikono ya polisi ni vigumu kukutana na waandishi wa habari na kuzungumza ukweli. Baada ya kuliona hilo nimeamua kukutana nanyi ili kuwaambia ukweli Waislamu wenzangu kuwa katika tukio hili mimi sihusiki hata kidogo na hata huyo anayetajwa kuwa kiongozi wa kundi simfahamu,” alisema Zahaki.
Alisema kutokana na matukio ya Mwembe Chai, Jeshi la Polisi lilikasirishwa na limekuwa likimfuatilia  kila hatua ili ipatikane nafasi ya  kumpa kesi ili wampoteze ulimwenguni.
“Ndugu waandishi wa habari, mimi miaka yote nipo hapa nchini, nina wake wawili ambao naishi nao. Ajabu ni kwamba Jeshi la Polisi linadai mimi nimerejea kutoka Ethiopia. Huo ni uzushi ambao wanajaribu kuutumia ili nionekane muhalifu wakati ni uongo mtupu”,  alisema Zahaki.
Zahaki aliongeza: “Jeshi la polisi wawe wa kweli. Wafanye utafiti wao kwa makini badala ya kuvamia watu kwa kuwa shuku kwani hatua hiyo itafanya kukamatwa kwa watu ambao hawana hatia jambo ambalo halitamuathiri mtuhumiwa peke yake bali litaathiri maisha ya watoto, wake na wazazi wake”.
“Mimi nilikuwa Sajenti katika kitengo cha ‘Crime Stoppers Unit’  -   Central Police. Tukio la Mwembe Chai lilivyotokea mimi nilikuwa ndio ‘in charge’. Nilitoa maelezo yangu kuhusu taarifa za tukio hilo lakini jeshi halikuridhika.  Wamenifukuzwa kwa aibu na sasa wananishughulikia nje ya Jeshi la Polisi”. Alilalamika Zahaki huku machozi yakimlenga lenga.
Ujumbe kwa Waislamu
Zahaki amewataka Waislamu wenzake kumuombea dua kwa mtihani huo ambao ameupata huku akiwahakikishia kuwa hajahusika katika uhalifu huo uliotekelezwa katika kituo cha Stakishari.
“Wa Llaah wa Billaahi sijahusika na uhalifu wa Stakishari, Mwenyezi Mungu anajua zaidi. Nitakwenda kuwahoji kwa nini wametaja jina langu na kulihusisha na mauaji yale, na pia  kwa nini wanadanganya umma wa Watanzania kuwa mimi nimerejea kutoka Ethiopia wakati nipo hapa nchini? Wana ajenda gani ya siri” alisema Zahaki.
Aidha, Zahaki alisema anataka Waislamu wajue ukweli wote hata akiwa ameshikwa na Jeshi la Polisi ama kuuliwa katika mazingira ya kutatanisha, wajue kilichomuua ni chuki kutokana na kusema kweli katika kadhia ya Mwembe Chai.
 Aibukia Jeshi la Polisi, akamatwa
Kama alivyoahidi kwa waandishi wa habari kuwa angekwenda kuhoji Jeshi la Polisi juu ya jina lake kuhusishwa na mauaji ya Stakishari, Zahaki  kweli alifanya hivyo . Lakini taarifa ambayo Jeshi la Polisi kanda maalum ya Dar es Salaam ilIitoa kwa waandishi wa habari ilisema  mtuhumiwa huyo alijisalimisha.
Akizungumza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alisema Mtuhumiwa Zahaki Ngai amejisalimisha kwa Jeshi la Polisi akiwa na wake zake wawili na kusema kuwa wale ambao bado hawajapatikana msako bado unaendelea.
Maneno hayo ya Kamishna Kova ni kama mwiba kwa Zahaki ambaye alishatangaza kuwa anaenda kuhoji kwa nini jina lake limetajwa na sio kujisalimisha. Kama alivyotabiri, inaonekana kama polisi wameendelea kupotosha umma.
Akizungumza na gazeti Imaan, Mwanasheria wa mtuhumiwa huyo alisema wanashangazwa na upotoshaji wa Kamanda Kova kwa umma wa Tanzania kwani Zahaki hakwenda kujisalimisha bali alikwenda kuuliza ukweli wa tetesi anazozisikia katika vyombo vya habari.
Kilindo alisema upotoshaji huo unakera na unaudhi kwani matamshi ya Kamishna wa polisi ni sawa na kuthibitisha kuwa ana uhakika  Zahaki ni mhalifu na hivyo kupewa kesi hiyo wakati yeye hakuhusika na kadhia hiyo.
Katika tukio ambalo polisi wanadai Zahaki alihusika, majambazi kadhaa yalivamia kituo cha polisi cha Stakshari na kuua watu saba majira ya saa 5 usiku, Julai 12, 2015. Mpaka sasa tayari watuhumiwa tisa wanahojiwa kuhusiana na tukio hilo.  

(Makala kwa hisani ya gazeti la Imaan Agosti 31 - Septemba 6, 2015)


No comments: