Sunday 11 September 2016

KITENDAWILI KATIKA KUTUNUKU MAJINA YA MITAA YA DAR ES SALAAM KWA WAPIGANIA UHURU WA TANGANYIKA




Mtaa huo hapo kwenye hiyo picha hapo juu zamani ukijulikana kama Somali Street. Katika miaka ya 1990 wakati Kitwana Selemani Kondo ni Meya wa Jiji alibadili baadhi ya majina ya mitaa na kuipa majina ya wazalendo walioacha alama katika historia ya kupigania uhuru wa Tangnayika. Lilikuwa wazo zuri isipokuwa kwa jambo moja nalo ni kule kutoa majina kwa baadhi na kuacha baadhi. Baya zaidi ni kule kuwaacha wale ambao michango yao ilikuwa mikubwa sana na kutunuku majina mitaa kwa wengine ambao michango yao haikuwa kwa kiwango kuzidi hao walioachwa. Mtaa wa Somali katika miaka ya 1950 wakati wa kudai uhuru wakiishi wazalendo wawili katika harakati za TANU – Omari Londo na Zuberi Mtemvu. Mchango wa Mtemvu ulikuwa mkubwa kuliko wa Londo lakini jina la mtaa amepewa Londo. Yawezekana Mtemvu kanyimwa heshima ile kwa kuwa alitoka TANU mwaka wa 1958 na kuanzisha chama chake cha Congress alipotofautiana na Nyerere katika suala la Kura Tatu.


Photo
Mtaa wa Somali kama ulivyokuwa katika miaka ya 1950/60

Aliyekaa mbele anatabasamu ni Omari Londo na nyuma yake ni Abdallah
Kassim Hanga na juu ya jukwaa ni Julius Nyerere
 Gerezani ulipo Mtaa wa Omari Londo kuna Mtaa wa Mbaruku. Mtaa huu ndiyo Mtaa aliokuwa akiishi Dossa Aziz mmoja wa waasisi wa TANU na mfadhili mkubwa wa harakati za kudai uhuru wa Tanganyika. Jina la mtaa halikubadilishwa na mtaa kupewa jina la Dossa. Lakini kitu cha ajabu na cha kusikitisha ni kuwa mtaa wa mbele yake uliokuwa ukijulikana kama Kisarawe Street umepewa jina la Yusuf Makamba. Mimi sijui mchango wake katika historia ya Tanganyika na wala sielewi kwa nini mtaa ule asipewe mzalendo yeyote yule katika wazee wa Dar es Salaam waliotoa mchango mkubwa katika kupinga ukoloni. 

Ndugu msomaji hebu soma kisa cha Mtaa wa Mshume Kiyate ambao alitunukiwa Mzee Mshume lakini mamlaka imekataa kuntunuku.


 


Ukweli ni kuwa Mtaa wa Mshute Kiyate haupo kwa sababu wahusika wamekataa kubadili kibao cha jina sasa yapata zaidi ya miaka 20. Kitwana Kondo alipokuwa Meya wa Jiji la Dar es Salaam ndiye aliyefanya mabadiliko ya majina ya mitaa kuwaenzi wazalendo waliopigania uhuru wa Tanganyika kwa kuipa majna yao ile mitaa waliokuwa wakiishi. Hivyo ndivyo Mtaa wa Kipata ujabadilishwa na kuitwa Mtaa wa Kleist Sykes, Mtaa wa Somali ukaitwa Omari Londo, Mtaa wa Aggrey ukaitwa Max Mbwana, Pugu Road ikaitwa Barabara ya Mwalimu Nyerere, Bi. Tatu binti Mzee akapata mtaa Ilala na Mtaa wa Tandamti ukabadilishwa jina na kuitwa Mtaa wa Mshume Kiyate. Lakini palizuka malalamiko kuwa kilichomsukuka Kitwana Kondo kubadili majina ni hisia za udini. Hii ni baada ya kuonekana wazalendo wengi waliopewa majina ya mitaa ni Waislam. Magazeti yakahoji ni michango gani wazalendo hawa walitoa? Kitwana Kondo katika mahojiano aliyofanya na marehemu Sarah Dumba wa Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) alijibu kwa kusema, ''Ikiwa hamjui michango ya watu hawa ulizeni mtaelezwa.''


Mtaa wa Kipata (Sasa Kleist Sykes)
Kleist Sykes (1894 - 1949)
Kulia wa pili ni Mshume Kiyate


Kushoto: Mwinjuma Mwinyikambi, Max Mbwana Julius Nyerere na Mshume Kiyate
Uchaguzi Mkuu wa 1962



Mzee Mshume Kiyate akimfariji Mwalimu Nyerere baada ya maasi ya wanajeshi
20 Januari 1964
Photo
Mtaa wa Mshume Kiyate katika mihangaiko ya kutafuta rizki nyakati za mchana wakati  wa kutafuta rizki

Photo
Mtaa wa Mshume Kiyate karibu na Soko la Kariakoo kama unavyoonekana hivi sasa

1 comment:

Kanungila Karim said...

Historia nzuri sana