Wednesday 15 March 2017

MSIBA WA GEORGE KAHAMA WAMKUMBUSHA MHARIRI WA RAIA MWEMA ABDULWAHID SYKES


Tahariri Raia Mwema 15 - 21, Machi 2007
Kushoto Tatu biti Mzee, Julius Nyerere na wa pili kulia Bi. Titi Mohamed
wakimsindikiza Nyerere Uwanja wa Ndege  safari ya kwanza UNO 1955
Baraza la Kwanza la Mawaziri 1961

Mhariri wa Raia Mwema katika toleo lake la 15 - 21, Machi 2007 katika tahariri yake kwa kumuadhimisha marehemu George Kahama atakaezikwa Alkhamisi ameeleza masikitiko yake kwa Tanzania kutokuwa na historia ya mashujaa wake. Mhariri kamtaja pamoja na wazalendo wengine Abdul Sykes kama mmoja wa wazalendo ambae historia ya mchango wake katika kupigania uhuru wa Tanganyika bado haujathaminiwa. 

Binafsi nimefarajika kuwa kumbe si mimi peke yangu ninayoona upungufu huu katika taifa letu.

Mara ya kwanza mwaka wa 1988 gazeti la Africa Events lililokuwa likichapwa London lilipochapa makala yangu, ''In Praise of Ancestors,'' na nikamtaja marehemu Abdul Sykes kwa sifa ya kuaisi chama cha TANU 1954, toleo zima lilikusanywa na kutolewa katika mzunguko.

Mambo hayakuishia hapo toleo la gazeti hilo lililofuatia ilichapwa barua kutoka CCM Makao Makuu Dodoma iliyoandikwa na kada mashuhuri wa wakati huo na aiyekuwa na cheo kikubwa katika Sekretariati ya Kuhamasisha Umma iliyokuwa na vitisho na dharau dhidi yangu. Kisa na kosa langu kumtaja Abdul Sykes na wazalendo wengine na kusema kuwa historia ya uhuru wa Tanganyika haiwezi kutenganishwa na mchango wa Waislam katika kupigania uhuru wa Tanganuyika. 

Alipokufa Dossa Aziz katika maziko yake Mlandizi hakuna katika viongozi wa CCM aliyekuwapo pale mazikoni aliyejua Dossa alikuwa nani kwa Mwalimu Nyerere wala kwa TANU yenyewe na kwa bahati mbaya sana Nyerere hakuhudhuria maziko yale. Labda angekuwapo angemueleza Dossa alikuwa nani kwake na kwa TANU.

Alipokufa Paul Bomani mambo hayakuwa tofauti na yale ya maziko ya Dossa Aziz. Hakuna katika viongozi wa CCM aliyejua mchango wa Bomani.

Hawa wazalendo watatu niliowataja hapa kwa uchache wote wanaunganishwa na sifa moja adimu sana. Hawa walitajirika katika ukoloni na TANU ilipoasisiwa ilikuwakua tayari wakiwa na fedha zao. Hawa hawakutajirikia katika TANU. Wazalendo hawa walitoa fedha nyingi kwa TANU katika kupigania uhuru wa Tanganyika.

Kwa kuhitimisha ningependa kusema kuwa hakika nimefarajika sana kuwa kumbe kuna wenzagu na wao wameona upungufu wa jambo hili.

Kwa kuitika mwito wa Mhariri wa Raia Mwema itapendeza kama katika jengo jipya la CCM pale Patrice Lumumba Avenue CCM ikaanza kutafuta historia ya mashujaa wetu na kuwaenzi angalau kwa kuweka picha zao na maelezo mafupi. 

Kizazi hiki cha leo kingependa kuona picha ya Sheikh Suleiman Takadir na maelezo yake ya mchango wake katika kudai uhuru wa nchi yetu, picha ya Saadan Abdul Kandoro, Hamza Mwapachu, Bi. Titi Mohamed na Tatu biti Mzee, Iddi Faiz Mafungo, Mshume Kiyate kwa kuwataja wachache na huko mikoani na wilayani haya yafanyike.

Hapo Makao Makuu ya CCM Dodoma ziwekwe picha za Omar Suleiman, Haruna Taratibu, Edward Mwangosi, Tanga zikwekwe picha za Abdallah Rashid Sembe, Bi. Mwanamwema, Hamisi Heri. Lindi picha za Salum Mpunga, Yusuf Chembera, Sheikh Yusuf Badi. Kilimanjaro waweke picha za Eikaeli Mbowe, Yusuf Olotu, Juma Ngoma, Mama Biti Maalim, Halima Selengia.

Bukoba waweke picha za Ali Migeyo, Suedi Kagasheiki, Abdallah Rutabanzibwa nk. nk.


Tusitishike na majna haya ya Kiislam kwani hii ndiyo historia yenyewe hatutoweza kuibadili.




Job Lusinde
Chifu Abdallah Said Fundikira
Mwalimu Kihere
Nyerere na Mshume Kiyate 1964

Robert Makange akiandika gazeti la TANU Mwafrika 1950s katikati

Kushoto Mwinjuma, Mwinyikambi, Max Mbwana Julius Nyerere na
Mshume Kiyate 1962

No comments: