Tuesday 27 June 2017

CHIEF EDWARD ANTHONY MAKWAIA WA BUSIYA

Chief Makwaia Mohamed Mwandu

Nimeona tangazo la Busiya Chiefdom katika mitandao ya kijamii na nikaangalia, ‘’clip,’’ yake. Hili ni tamasha linalofanyika hapo Busiya kulipokuwa na uchifu wa Makwaia. Mwalimu Nyerere alifuta uchifu katika baada ya uhuru wa Tanganyika lakini taratibu uchifu unarejea kwa kuona umuhimu wa kuenzi asili za watu na utamaduni wao. Uchifu huu hauna mamlaka ya utawala ila heshima na kumbukumbu.


Chief Michael Lukumbuzya

Historia ya Mwalimu Nyerere na machifu waliokuwapo Tanganyika toka enzi na enzi, kama baba yake Chief Edward Makwaia, Chief David Kidaha Makwaia, Chief Abdallah Said Fundikira, Chief Haruna Msabila Lugusha, Chief Thomas Marealle, Chief Makongoro, Chief Abdiel Shangali, Chief Kunambi, Chief Majebele, Chief Adam Sapi Mkwawa, Chief Ngua na mkewe Mwami Theresa Ntare, Chief Mang’enya, Chief Michael Lukumbuzya na wengineo ni historia yenye msisimko wa kipekee kabisa.


Chief Thomas Marealle

Nimebahatika katika maisha yangu kufahamiana na baadhi ya hawa machifu katika siku zao za mwisho wa maisha yao na pia kufahamiana na watoto wao kwa karibu na kutoka kwao nimejifunza mengi katika yale yaliyokuwa katika fikra za wazee wao na yale waliyokuwanayo wao wenyewe binafsi.


Kulia: Abraham Ally Sykes na Kibo Marealle nyumbani kwa Mwandishi Tanga1999



Kuwa hivi sasa uchifu wa Makwaia wa Busiya Usukumani umerejea hakika ni kitendo cha kupigiwa mfano.

Kumbukumbu nyingi za machifu waliokuwapo aidha zimekufa kabisa au hazipo na zile zilizokuwapo ziko taabani.

Chief Abdallah Said Fundikira

Labda nieleze kwa nini nimeguswa na uchifu Mkwaia wa Busiya.

Nimeguswa na uchifu wa Busiya kwa kuwa kiongozi wa uchifu huu ni rafiki yangu toka utotoni.
Nimejuana na Chief Edward Anthony Makwaia mwaka wa 1967 sasa imepita miaka 50, yaani nusu karne.

Nilimfahamu Edward pale nilipoingia St. Joseph’s Convent mwaka wa 1967 kujiunga na elimu ya sekondari na tulisoma darasa moja hadi mwaka wa 1970. Yeye alikuwa anatolea Salvatorian College na mimi Kinondoni Primary School.

Katika miaka hii minne ya shule tuliingiliana sana na Edward akawa rafiki yangu kipenzi na kupitia kwake nikajuana na jamaa zake wengi kama akina Mwapachu na akina, Yunge na Gordon. Lakini katika maajabu ya maisha ni kuwa hata kabla sisi hatujazaliwa wazee wetu kwa njia za ajabu kabisa walikuwa na uhusiano wa hapa na pale.

Mmoja katika ukoo wa kina Yunge aliingiliana sana na wazee wangu katika miaka ya 1950 na nina picha nilipiga na Kapufi Yunge sote tukiwa watoto ingawa Kapufi alikuwa kanitangulia labda kwa miaka miwili hivi. Picha hii ninayo katika maktaba na nikiitia mkononi nitaiweka hapa. Picha hii ilikuwa ukutani kwa mama yangu mkubwa Bi. Mwanaisha bint Mohamed kwa kipindi chote cha maisha yake na kila alipokuwa akiizungumza ile picha alikuwa akimwita Kapufi, ‘’Chapa Ng’ombe,’’ kwa ajili ya ule Usukuma wake kwani Wasukuma ni wafugaji wakubwa wa ng’ombe.

Picha hii ilipigwa mwaka wa 1956 katika studio ya Gomes, iliyokuwa Acacia Avenue (Baada ya uhuru 1961 mtaa ukaitwa Independence Avenue na sasa ni Samora Avenue. Huyu Gomes ndiye aliyepiga ile picha maarufu ya waasisi wa TANU mwaka wa 1954). 


Waasisi wa TANU
Picha iliyopigwa na Gomes 7 Julai, 1954


Katika mwingiliano huu nikamkuta Edward ambae siku zile tulizoea kumwita Teddy akiwa na udugu na jamaa zangu wengi, mmoja wa ‘’cousin sister,’’ wake Lilian amabe tulizoea kumwita Lilly akiwa ni binti ya Abbas Sykes. Mimi, Teddy, Lily (ambae tulikuwa sote St. Josephs), Kleist Abdul Sykes, Ebby Abdul Sykes, Monalisa na Alma Ally Sykes ikawa sote tumekuwa pamoja utotoni tukiwa  na watoto wa koo mashuhuri katika Dar es Salaam ya wakati ule kama akina Lyabandi, Abbas Max, Sykes, Tsere, Singano, Bizuru, Msikinya, Lukindo, Mkwawa, Maharage, Masayanyika, Mang’enya, Muhuto, Fritsch, Kondo, Kafumba, Mzena, Bomani, Kahama, Kharusi na nyingineo nyingi. Kundi hili ambalo ndilo rika langu sasa sote sisi ni watu wazima na umri wetu wastani ni miaka 60.


Kulia: Balozi Mohamed Maharage Juma, Balozi Anthony Cheche, Balozi Patrick Tsere (mtoto wa Dr. Luciano Tsere)
Dr. Tsere ni mmoja wa madaktari watano ambao walisaidia sana kuijenga TAA baada ya Vita Kuu ya Pili, wengine ni Dr Vedasto Kyaruzi, Dr Wilbard Mwanjisi, Dr Michael Lugazia na Dr Joseph Mutahangarwa

Nyuma kulia ni Haitham ''Angela Davis'' Rashid, Mwandishi na Kamili Mussa.
Kushoto waliokaa ni Stella Emanuel. Esther Mzena na Wendo Mwapachu hii ilikuwa picnic tulifanya
Kigamboni kwenye nyumba ya mapumziko ya Rais Nyerere na aliyetupeleka hapo ni Magombe Makongoro, 1968
Katika familia hizi kuna historia kubwa ambazo kwa wakati ule wa utoto sikuzijua hadi nilipofika utu uzima. Historia ambazo zinakwenda na historia ya Tanganyika kuanzia kupigania uhuru wa Tanganyika na Zanzibar hadi kufikia mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka wa 1964. Historia ya mauaji kwa Zanzibar hadi vifungo vya siasa na kudhulumiwa kwa mali kote Tanganyika na Zanzibar.



Kulia: Ali Muhsin Barwani, Dr. Idarus Baalawy, Mohamed Shamte, Juma Aley na Ibun Saleh


Ilinichukua miaka mingi kuja kuijua historia ya ukoo wa Kharusi, Ibun na Shamte wa Zanzibar ingawa marafiki wawili wa baba yangu, Abdulaziz Twala na Jaha Ubwa walikuwa wameuawa baada ya mapinduzi. Ilinichukua miaka mingi pia kuja kuijua historia ya Chief Kidaha Makwaia. Nilipigwa na bumbuazi siku nilipoambiwa kuwa Abdul Sykes alimtaka Chief Kidaha Makwaia awe Waziri Mkuu Tanganyika itakapokuwa huru kwa Chief Kidaha kuwa rais wa TAA kisha waunde TANU yeye Chief Kidaha akiwa rais wa TANU. Hii iikuwa katika miaka ya 1950 wakati ule Chief Kidaha mjumbe wa LEGCO.


Kulia: Chief Edward Anthony Makwaia wa Busiya alipokwenda kumpa pole Kleist Sykes (kushoto) alipofiwa na mdogo wake Adam Abdulwahid Sykes. Kiasi cha nusu karne iliyopita baba zao watu hawa walikaa mara kadhaa wakijadili namna bora ya kuwaondoa Waingereza Tanganyika. Wakati ule Chief David Kidaha Makwaia alikuwa mjumbe wa LEGCO na Abdul Sykes alikuwa Katibu na Kaimu Rais wa TAA. Mengi ya mazungumzo haya yakifanyika nyumbani kwa baba yake Kleist.  Hakika dunia inazunguka.

Ilinichukua pia miaka mingi kuijua kwa undani historia ya ukoo wa Sykes lau kama hawa walikuwa jamaa wa karibu sana na wazee wangu kuanzia mababu zangu katika miaka ya 1920. Kwa hakika ilinichukua miaka mingi kuijua historia ya babu yangu mwenyewe katika kupigania uhuru wa Tanganyika na kupigania haki za wafanyakazi kupitia vyama vya wafanyakazi. Wakati ule sikuweza kutambua kuwa ule urafiki niliyokuwa nashuhudia baina ya Edward Makwaia na Kleist Sykes umetoka mbali kwa baba zao wakati wa harakati za kudai uhuru wa Tanganyika. Sikuweza kwa wakati ule kujua kuwa ule ukaribu wa Wendo Mwapachu na Kleist ulitoka huko nyuma pia.


Kulia: Asya Kharusi na Sambayawo Nyirenda hawa wote ni madaktari wa binadamu.
Baba yake Sambayawo, Alexander Gwebe Nyirenda ndiye aliyepandisha bendera ya Tanganyika Mlima
Kilimanjaro usiku wa uhuru
Kwa miaka ile ya utoto sisi watoto kutoka familia hizi sote tulikuwa wamoja tukicheza pamoja wakati mwingine watoto wa washindi na washindwa au ukipenda watoto wa waliodhulumu haki za watu na wadhulumiwa tukiwa wamoja bila kujua yale yaliyopitikana siku za nyuma kati ya wazee wetu na watawala waliokuwa madarakani.Ilinichukua miaka mingi kujua kuwa eneo lote la Upanga hadi kufikia Selender Bridge hadi Ikulu ilikuwa hodhi ya ukoo waTambaza hadi kufikia miaka ya 1800 na wakanyang'anywa na Wajerumani na hadi leo kuna makaburi ya mababu zao ndani ya Ikulu. Katka miaka ya 1980 waliamua kutoa ardhi iliyokuwa makaburi ya wazee wao Upanga ujengwe msikiti uliopewa jina, ''Masjid Maamur.'' Huu uliongeza misikiti inayowahusu Dar es Salaam kuwa mitatu wa kwanza ukiwa Masjid Mwinyikheri Akida ambao (una zaidi ya miaka 100 na ndiyo msikiti wa kale kupita yote Kariakoo) na Masjid Tambaza.

Kama ulivyo wastani wa umri wetu miaka 60 na miaka ya utoto wetu ilikuwa katika 1960s na Waingereza waliipa jina miaka hii wakaiita, ‘’The Roaring 60s,’’ na kwa hakika hii ilikuwa miaka ya aina yake. Tulikulia katika mazingira na utamaduni wa aina yake. Waingereza walikuwa wameondoka na wamewaachia utawala wazee wetu. Wazee wetu waliathirika na sisi watoto wao pia. 


Waliokaa kulia: Yusuf Zialor, Wendo Mwapachu
Kulia waliosimama ni Abdallah Tanbaza Abdul Mtemvu na Abdallah Mggambo

Palikuwa na aina mpya ya maisha ambayo kwa kiasi fulani yalitia afueni kwa wazee wetu kwa kukamata nafasi za kazi ambazo zamani zilikuwa zikishikiliwa na Wazungu na Waasia.




Wazee wetu walikuwa wanapumua kutokana na kazi ngumu ya kupigania uhuru katika miaka ya 1950.


|Chief David Kidaha Makwaia

Hata hivyo katika hali hii palikuwapo pia na majeruhi ya harakati za ukombozi wa Tanganyika. Baadhi ya majeruhi hawa walikuwa machifu ambao jana tu walikuwa watu wenye hadhi zao katika jamii lakini ghafla baada ya uhuru kupatikana na Mwalimu Nyerere kufuta uchifu, machifu hawa wakajikuta katika hali ambayo hawakuitegemea kamwe.

Hii ni historia ya pekee inayohitaji ipatiwe nafasi iandikwe.

Juu ya haya yote mmoja kati yetu watoto tuliolelewa katika miaka ya 1960 wakati Tanganyika inapata uhuru wake kutoka kwa Waingereza, leo ni Chief wa Busiya, utawala uliokuwa na nguvu katika wakati wake.

Vipi Edward na watu wa Busiya wameweza kurejesha uchifu wa mababu zao, vipi waliweza kumtawaza  Chief Edward Anthony Makwaia na mengi mengine nadhani iko siku yataelezwa.

Kwa sasa muhimu ni kuwa kila mwaka wakati wa Saba Saba, Wasukuma wa Busiya huwa wanafanya tamasha kuhuisha utamaduni wao na uchifu uliozaliwa upya wa Busiya.


Chief Edward Anthony Makwaia katika vazi la kichifu

Chief Edward Anthony Makwaia akicheza ngoma ya Kisukuma
2016

Kushoto aliyepiga magoti ni Mama Mary Mackeja mama yake Edward Makwaia
siku ya sherehe ya kuzaliwa kwake kulia wa kwanza ni Mwandishi, William Mfuko, Juma Volter Mwapachu na nyuma ya Mama Mackeja ni Wendo Mwapachu
1967

Kulia waliochutama: Edward Anthony Makwaia, Salma Bhatia, Asya Kharusi, Razia Bhatia, Iddi Mvule, David Gabba,
Waliosimama kulia: Mwandishi, Shayo, Maximillian Mafuru
Kulia waliosimama: Gulamabbas Jivraj, Israel, Charles Mesquita


Picinic Form One D St. Joseph's Convent 1967 Kigamboni Beach
Kulia waliokaa: Iqbal Bapumia, Salma na Razia Bhatia wengine majina sikumbuki
Kulia waliosimama: David Gabba nyuma ya Daivid ni Edward Makwaia anefatia jina sikumbuki baada yake ni Sambayawo Nyirenda, Fortunata, Zariha Juma, Wun Siang Chou, Shenaz na wa mwisho ni mwalimu wetu wa darasa Miss Kindy.
Nyuma kabisa baada ya Edward Makwaia ni Khalid Abdallah

Kulia: Edward Makwaia, Willliam Mfuko, Mwandishi na Khalid Abdallah

Kulia: Mwandishi, Yusuf Zialor, Kleist Abdulwahid Sykes, Bubby, Abdallah Tambaza waliokaa kulia ni Abdul Mtemvu, Wendo Mtega Mwapachu na Kessy 

Kushoto Lilian Abbas Sykes akizungumza na Jaji Mark Bomani mwisho kulia ni Mohamed Chande Jaji Mkuu Mstaafu
Kulia waliokaa: Shayo, Iqbal Bapumia
Kulia waliosimama: David Gabba, John Gondwe, Sambayawo Nyirenda, Khalis Abdallah, Abdul Yusuf, Shaib Salum
Nyuma: Maxmillian Mafuru, Asya Kharusi Jennnifer Gordon, Mwandishi na Edward Makwaia

Mwandishi katika sherehe ya siku za kuzaliwa Iqbal Bapumia ''class mate,'' 1969
Picha kapiga Iqbal

No comments: