Sunday 17 September 2017

HALAL BADR, TAWASWIL NA VISOMO VILIVYOSOMWA WAKATI WA KUDAI UHURU WA TANGANYIKA


Wakati nafanya utafiti wa kitabu cha Abdul Sykes nilikutana na matokeo manne ambayo wananchi walijikusanya na kufanya visomo au dua kujikinga na dhulma za ukoloni wa Waingereza. Katika matukio haya manne ya kumuomba Mungu ni tukio moja tu ndilo wafanyaji kisomo walichobainisha kuwa inayosomwa ni ‘’Halal Badr’’ neno ambalo hivi sasa limekuwa maarufu midomoni mwa watu wengi baada ya kuelezwa kuwa kutasomwa Halal Badr makhsusi kufuatia jaribio la kumuua Mbunge wa Singida Mashariki, Mheshimiwa Tundu Lissu.

Nitarudi nyuma kiasi cha nusu karne na zaidi kuangalia nafasi ya visomo katika kutafuta haki. Nitaaanza kwa kueleza mazingira yaliyokuwapo wakati wa ukoloni hadi kusababisha wananchi kumgeukia Mungu na kutaka msaada wake na hivyo kusoma Halal Badr.

Nakuwekea msomaji wangu yale niliyoandika katika kitabu cha Abdul Sykes, kitabu ambacho ndani yake nimejaribu kueleza historia ya uhuru wa  na kuandika kuhusu Halal Badr ili kwa yule ambae ni mgeni katika mambo haya apate picha kamili na Tanganyika ili uweze kuona ilikuwa na kujua ni wakati gani wananchi waliamua kufanya dua iwe Halal Badr au kisomo kingine kama kinga yao dhidi ya nguvu ambayo wao waliona ni Mungu pekee ndiye angeliweza kuwapa nusra.

Labda tujiulize imekuwaje leo baada ya zaidi ya nusu karne wananchi wanarejea katika mbinu ambazo wengi wanaona kuwa kuzirejea tena katika Tanzaia huru ni kitu ambacho kidogo kinashangaza hasa kwa kuwa dini kama inavyoelezwa kuwa haina nafasi katika uendeshaji wa serikali.

Naanza kwa kukuwekea hapo chini mara yangu ya kwanza nilipokutana na huu makakati ambao kwa hakika ulikuwa mpya katika mbinu za kudai haki kwa kukueleza vuguvugu la makuli katika bandari ya Dar es Salaam pale walipoamua kupambana na dhulma za wakoloni kwa kusoma Halal Badr mwaka wa 1947:

‘’…kidogo kidogo Kleist alianza kumkabidhi Abdulwahid kazi za African Association na mara akawa msaidizi wa baba yake katika siasa za Dar es Salaam. Ilikuwa katika kutimiza haya ndipo Abdulwahid akajikuta anahusika na ule mgogoro wa makuli ulioibuka bandarini Dar es Salaam ambao ulikuwa ukichemka pole pole chini kwa chini kwa muda mrefu tangu kumalizika kwa vita. Hatimaye, Abdulwahid alihusika na harakati za siri za wafanyakazi bandarini ambao, wakiwa wamechoshwa na sheria za kazi za ukandamizaji na wakiwa wamechoka kunyonywa na makampuni ya meli, walikuwa wanapanga kuitisha mgomo.

Chama cha African Association ndicho kiliwakilisha maslahi ya wananchi wa Tanganyika na kimya kimya kiliunga mkono zile harakati za chini kwa chini za wafanyakazi katika kutafuta haki zao. Abdulwahid, kijana mdogo mwenye elimu na akiwa karibu zaidi na uongozi wa African Association kuliko Mwafrika yoyote pale mjini, alichaguliwa kuongoza harakati za tabaka la wafanyakazi zilizokuwa zinaibuka. Haya ndiyo mambo serikali ya kikoloni ilihofia na ndiyo ilikuwa sababu ya kumfanyia khiyana asiingie Makerere. Utawala wa kikoloni ulifahamu kuwa msukumo wa Kleist na mwanae aliyeelimika ungeipa Tanganyika uongozi uliokuwa unakosekana Tanganyika na pengine hata ndani ya Al Jamitul Islamiyya.

Ili kuifanya serikali iwasikilize mahali ambapo hapakuwa na sheria za kazi, ilibidi iwekwe mikakati ambayo ingeifanya serikali iweke sheria hizo katika vitabu vyake. Kamati ndogo ya siri iliundwa na Abdulwahid akatiwa ndani ya kamati hiyo ili kuongoza mgomo uliokusudiwa. Kazi ya kamati hiyo ilikuwa kupanga na kuratibu mikakati ya kuitisha mgomo ambao ungelisaidia katika kuondoa ile dhulma iliyokuwepo. Makuli waliitisha mkutano pembeni kidogo mwa mji, mahali palipokuwa pakijulikana kama ‘’Shamba kwa Mohamed Abeid,’’ katika bonde la Msimbazi. Sehemu hii ilichaguliwa makhususi mbali na macho ya watu ili ipatikane faragha. Makuli walikula kiapo na kusoma, ‘’Ahilil Badr,’’ ili kujikinga na unafiki, usaliti pamoja na shari ya vizabizabina  wangeokataa kugoma. Ubani ulifukizwa na Qur’an ilisomwa. Wakijikinga na kiapo hicho cha mashahidi wa vita vya Badr na huku wakichochewa na ushujaa wa mashahidi waliokufa katika katika  vita vya Badr wakipigana na washirikina wa Makka wakiwa pamoja na Mtume Muhammad (Rehema na Amani za Mwenyezi Mungu Ziwe Juu Yake), makuli walichagua tarehe 6 Septemba, 1947 kuwa ndiyo siku ya kuanza  mgomo wao.

Mapema asubuhi moja kile kilichoanza kama mipango ya siri dhidi ya  makampuni ya Wazungu bandarini, kililipuka na kuwa mapambano ya dhahiri. Watu katika mitaa jirani ya alipoishi akikaa Abdulwahid walikuwa hawajatoka vitandani mwao alifanjiri moja waliposikia vishindo na makelele vimetanda mtaani. Makuli, baadhi yao wakiwa vidari wazi, walikuwa wameizingira nyumba ya Kleist, wakipiga makelele wakimtaka Abdulwahid atoke nje. Makuli wale walipiga kwata njia nzima kutoka bandarini huku wakitoa maneno ya kupinga ukoloni na  wakiimba kupandisha morali zao. Tukio hili halikuwa na kifani. Ilikuwa ni mara ya kwanza nchini Tanganyika kwa wananchi kushuhudia katika mitaa ya Dar es Salaam uasi wa dhahiri kama huo dhidi ya serikali ya kikoloni. Abdulwahid, wakati ule kijana mdogo kabisa, akichungulia kupitia dirisha la chumba chake alichokuwa amelala, alishangazwa kuona umati mkubwa wa watu nje ya nyumba yao. Aliweza kuwatambua baadhi ya wenzake katika kamati ile ya siri iliyokuwa inapanga mipango ya mgomo. Alipotoka nje kuonana nao makuli wenye hasira walimfahamisha kuwa mgomo ulikuwa umeanza na wasingerudi kazini hadi madai yao yote yamekubaliwa…’’

Kisomo kingine nilichokutana nacho wakati wa kudai uhuru wa Tanganyika kilifanyika Lindi na kisomo hiki kilifanywa na Sheikh Yusuf Badi lakini kwa kauli ya mpashaji habari wangu kisomo hiki kilikuwa Tawasul na katika waliohudhuria kwa kutajiwa majina yao walikuwa Suleiman Masudi Mnonji na  Bi. Sharifa bint Mzee:

Bi. Shariffa Bint Mzee

‘’Nyerere aliporudi Lindi mwaka 1959, TANU ilikuwa ina nguvu sana na ilikuwa imekumba kila mtu. Wale watumishi wa serikali wengi wao wakiwa Wakristo, walio kuwa wakiibeza  TANU mwaka 1955 kwa sababu ilikuwa ikiongozwa na Waislam ëwasiokuwa na elimu,í ukweli ulikuwa umewadhihirikia na sasa walikuwa wakionyesha heshima kwa chama. Hawakuwa na khiyari na ilibidi waonyeshe heshima kwa sababu bwana mwenyewe, yaani serikali ya kikoloni, ilikuwa na heshima kwa TANU. Serikali ilikuwa imetambua kuwa dhamiri ya watu ya kukataa kutawaliwa haiwezi tena kupuuzwa. Nyerere alikuwa amelihutubia Baraza la Udhamini la Umoja wa Mataifa mara mbili, mara ya pili ikiwa mwaka 1957. Ujumbe wa TANU ulikuwa wazi, watu wa Tanganyika walikuwa tayari kujitawala. Kila siku zilivyopita ndivyo TANU ilivyopata nguvu. Rashidi Salum Mpunga, dereva wa lori, aliweza kumshawishi na akafanikiwa kumuingiza TANU mmoja wa masheikh wenye kuheshimiwa sana mjini Lindi na mshairi maarufu, Sheikh Mohamed bin Yusuf Badi. Sheikh Badi alipoingia TANU kwa ajili ya heshima yake na kukubalika na watu, idadi kubwa ya Waislam walimfuata na kukata kadi za TANU. Nyerere alipokuja Lindi kujadili tatizo la kura tatu na uongozi wa Jimbo la Kusini, Sheikh Yusufu Badi alimpokea Nyerere na madras yake, wanafunzi wakimwimbia Nyerere kasda na kumpigia dufu. Kuanzia hapo sasa kila mtu alijiunga na TANU. Si Mponda wala Kanisa lilikuwa na uwezo wa kupambana na TANU kwa wakati ule. Polepole lakini na kwa kwa uhakika, TANU ilingia ndani ya maeneo ya Kikristo huko Songea, Masasi, Tunduru na Newala, nyumbani kwa Yustino  Mponda.
  
Lakini matukio mawili ya kumbukumbu kubwa yalikuwa katika safari ya pili ya Nyerere alipozuru tena Jimbo la Kusini. Kumbukumbu ya kwanza ilikuwa tawaswil aliyosomewa Nyerere na Sheikh Yusuf Badi mwenyewe pamoja na Waislam aliowachagua yeye sheikh mwenyewe maalum kwa hafla hiyo, pamoja na waliochaguliwa na masheikh wengine.’’

Kisomo kingine na hiki ndicho maarufu ni kile kilichofanywa nyumbani kwa Jumbe Tambaza Upanga ambacho Mwalimu Nyerere mwenyewe amekieleza.

Kisomo cha nne kilifanyika Mnyanjani, Tanga mwaka wa 1958 wakati TANU ilipokuwa inakabiliwa na tatizo la Kura Tatu:

‘’Siku kadhaa kabla ya kusafiri kwenda Tabora kwenye ule mkutano mkuu wa mwaka wa TANU, Nyerere na Amos Kissenge, Kaimu Katibu Mwenezi wa TANU, walisafiri kwenda Tanga kushauriana na uongozi wa Kamati Kuu ya Taifa ya TANU Tanga kuhusu matatizo yaliyoletwa na Uchaguzi wa Kura Tatu. Mkutano huu baina ya Nyerere, Kissenge na ule uongozi wa Tanga ulikuwa wa siri sana. Tanga iliwakilishwa na Hamisi Heri, Mwalimu Kihere, Abdallah Rashid Sembe, Ngíanzi Mohamed, Mustafa Shauri na Abdallah Makatta. Nyerere alizungumza waziwazi na kwa ithibati ya moyo wake. Nyerere alikiambia kikao kile kuwa amekuja Tanga kuomba wamuunge mkono kwa sababu ilikuwa ni matakwa yake TANU lazima ishiriki katika ule uchaguzi wa kura tatu uliokuwa unakaribia hata masharti yakiwaje. Nyerere aliuambia uongozi wa Tanga uliokuwa ukimsikiliza kwa makini kuwa alikuwa amekuja kwao kwa sababu watu wa Tanga wanajulikana kwa ufasaha wa lugha na kwa uwezo wao wa kuzungumza vizuri. Nyerere alisema angehitaji hiki kipaji adimu cha watu wa Tanga kuunga mkono msimamo wake huko Tabora. Nyerere alitoa hoja kwamba TANU lazima iingie katika uchaguzi kwa sababu kuususia ni sawasawa na kukipa chama hasimu, UTP ushindi bila jasho kuingia katika Baraza la Kutunga Sheria. TANU ingedhoofika na hivyo ingekosa sauti katika maamuzi yatakayotolewa na serikali katika  siku zijazo.

Sheiikh Abdallah Rashid Sembe

Kufichuka kwa msimamo wa Nyerere wa kutaka TANU iingie kaatika kura tatu kulishtua uongozi wa Tanga. Majadiliano makali yalifuata uongozi wa Tanga ukionyesha upinzani wao kwa msimamo wa Nyerere. Baada ya majadiliano ya muda mrefu Nyerere alifanikiwa kuwashawishi wote wawili, Hamisi Heri na Mwalimu Kihere ambao ndiyo walikuwa wapinzani wakubwa wa msimamo wa Nyerere na uchaguzi wa kura tatu. Nyerere aliutahadharisha uongozi wa Tanga kuwa agenda ya kura tatu itakapokuja anatabiri kupata upinzani mkali kutoka katika majimbo. Huko Tanga kwenyewe, TANU ilikuwa ikikabiliwa na upinzani mkali kutoka UTP na serikali. Matawi kadhaa yalikuwa yamepigwa marufuku.   UTP ilikuwa na nguvu Tanga kwa sababu wanachama wake wengi walikuwa wakimiliki mashamba ya mkonge katika jimbo hilo. Kwa ajili hii chama kilikuwa kinaelemewa na mashambulizi kutoka wa wapinzani. Wakati huo Tanga ilikuwa imetoa viongozi wenye uwezo lakini wote walikuwa wamehamishiwa makao makuu mjini Dar es Salaam. Wapangaji mikakati wazuri kama Peter Mhando alikuwa amehamishiwa Dar es Salaam na kutoka hapo alipelekwa Tabora ambako si muda mrefu akafa. Elias Kissenge vilevile alihamishiwa makao makuu kushika nafasi ya Katibu Mkuu wa TANU baada ya Oscar Kambona aliyekuwa ameshika nafasi hiyo kwenda Uingereza kwa ajili ya masomo. Uongozi wa TANU Tanga hata baada ya kujadili mbinu waliyopanga na huku Nyerere akielekeza mikakati ambayo Mwalimu Kihere na Abdallah Rashid Sembe wataitekeleza Tabora, bado uongozi ule ulikuwa na wasiwasi wa mafanikio ya mpango huo. Kwa ajili ya wasiwasi huu, viongozi wa TANU wa Tanga walimuomba Nyerere wawe pamoja ili ifanywe tawaswil waombe msaada wa Allah awape ushindi dhidi yaa vitimbi vya Waingereza. 

Maili tatu kutoka Tanga kipo kijiji cha Mnyanjani ambako kulikuwako na tawi la TANU lililokuwa na nguvu sana likiongozwa na Mmaka Omari kama mwenyekiti na Akida Boramimi bin Dai akiwa katibu. Mmaka alikuwa kijana aliyekuwa akiendesha mgahawa pale kijijini na Akida bin Dai alikuwa mwashi. Akida aliongoza tawi la vijana wa TANU ambalo baadae lilikuja kujulikana kama Tanga Volunteer Corps (TVC). TVC ilikuwa sawasawa na Bantu Group, ambayo wakati huo ilikuwa imekwishaanzishwa huko Dar es Salaam na Tabora. Vikundi hivi mbali na kufanya shughuli za propaganda na kuhamasisha wananchi halikadhalika viliifanyia TANU ujasusi. Nyerere na Kissenge walichukuliwa hadi Mnyanjani na tawaswil ikasomwa. Waliohudhuria kisomo hicho  walikuwa Abdallah Rashid Sembe, Sheikh Dhikr bin Said, Mzee Zonga, Hemed Anzwan, Salehe Kibwana aliyekuwa mshairi maarufu, Akida Boramimi bin Dai na Mmaka Omari. Aliyechaguliwa kusoma Quran Tukufu alikuwa mjomba wa Mwalimu Kihere, Sheikh Ali Kombora…’’


Mwalimu Kihere

Kipo kisomo kilifanywa na wafanyabiashara wa Soko la Kariakoo mwaka wa 1954/55 wakimnuia Town Clerk Mwingereza ambae alikuja Kariakoo Market kukamata kadi za TANU ambazo Abdul Sykes alikuwa kaziweka ofisini kwake na akiziuza pale sokoni. Ilikuwa Abdul apoteze kazi yake kama Market Master. 

Wazee wa pale sokoni walisoma Halal Badr. 
In Shaa Allah iko siku nitakieleza hiki kisa.

Shariff Abdallah Attas na Mzee Kisaka waliokuwa wakifanya kazi chini ya Abdul Sykes walikifahamu vizuri kia hiki.

No comments: