Sheikh Matimbwa,
Tumekushukuru kwa kutuwekea, ''clip,'' adhim ya Aga
Khan alipokuja Tanganyika mwaka 1956.
Nimeingia maktaba ili nai nichangie kitu katika
mambo ambayo Waismailia, yaani Aga Khan walifanya katika kusaidia Waislam wa
Tanganyika.
Katika miaka ya 1930s Al Jamiatul Islamiyya fi
Tanganyika walikuwa wanajenga shule ambayo sote tunaijua lakini hela zilikuwa
tatizo jengo likawa limechukua muda mrefu kukamilika.
Sababu ya kujenga shule hii ni kuwa wazee wetu
na wao walitaka wawe na mahali pa kuwasomesha watoto wao kuepuka vijana wao
kubatizwa katika shule ambazo serikali ya kikoloni iliziweka mikononi kwa
kanisa.
Kleist akiwa kiongozi wa Al Jamiatul Islamiyya
fi Tanganyika alitambua mapema sana kuwa tatizo kubwa lililokuwa likiwakabili
Waislam ilikuwa ni kukosa elimu ambayo serikali ya kikoloni iliwaachia
wamishionari waisimamie.
Si kama Waislam hawakuwa wanatambua faida ya
elimu kwa watoto wao. Wazazi wengi walichelea kuwapeleka watoto wao shule kwa sababu wamishionari
walichukua fursa hiyo kuwabatiza. Kuliko kwa watoto wao kutolewa katika Uislam
na kuwa murtad, wazazi wengi waliamua kuisamehe elimu yenyewe kabisa.
Kleist aliona kuwa ufunguo wa tatizo hilo kwa
Waislam ilikuwa ni kuanzisha shule zao wenyewe ambazo zitasomesha Qur’an pamoja
na masomo mengine.
Wakati ule, na hata hivi sasa, Qur’an ilikuwa
ikisomeshwa kwa mtindo wa asili ambapo mwanafunzi anakaa chini sakafuni mbele
ya maalim akiwa na ubao wake na juzuu.
Katika madras kuchapa viboko, kwa jina maarufu mkambaa,
ndiyo ulikuwa mtindo wa kusomeshea. Kleist hakuona sababu kwa nini Qur’an nayo
isisomeshwe kama elimu nyingine, wanafunzi wakiwa madarasani wakikaa katika
madawati.
Alilitoa wazo hili kwa rafiki zake akashauri
madras ipanuliwe ili masomo mengine yasomeshwe pamoja na Uislam.
Ushauri huu ulijadiliwa kati ya Kleist, Ali
Kiro, Maalim Popa Saleh na Shariff Salim. Wakitambua kazi kubwa iliyokuwa
ikiwakabili, waliamua waanze hiyo shule kwa kidogo kidogo kwa awamu. Nyumba
itakayokuwa shule ya muda ilitafutwa na wanafunzi wakaanza kusoma.
Kati ya walimu wa mwanzo wa shule hiyo walikuwa
Mzee Ali Comorian na Sheikh Abdallah Idd Chaurembo ambao walikuwa kati ya
wasomi wa Kiislam waliokuwa wakiheshimika.
Wazazi wa Kiislam waliombwa wachange fedha ili
jengo la kudumu lijengwe.
Al Jamiatul Islamiyya ikawa inapita nyumba hadi
nyumba ikusanya michango kutoka kwa Waislam.
Bahati nzuri mwaka wa 1936 Aga Khan alitembelea
Tanganyika na akafahamishwa kuhusu ujenzi wa shule ile.
Katika hafla ile mtoto aliysoma risala kwa Aga
Khan alikuwa Abdul Sykes akiwa na umri wa miaka 12.
Marehemu Kanyama Chiume amenihadithia kuwa
wakati huu alipofika Aga Khan Tanganyika yeye alikuwa anasoma Shule ya Kitchwele
na alikuwa katika bendi ya shule iliyompokea yeye akipiga, ‘’triangle,’’ na
alinieleza kuwa picha yake yeye akipiga, ‘’triangle,’’ ilitokea katika gazeti.
Aga Khan alitoa fedha na shule ikajengwa New
Street si mbali sana na ilipokuwa ofisi ya African Association.
Kleist akawa katika kamati ya ujenzi akikagua
kazi hadi ujenzi ulipokamilika. Hii ni moja kati ya shule za mwanzo kujengwa na
Waislam wa Tanganyika. Jengo la Al Jamiatul Islamiyya lipo limesimama hadi leo
kama ushahidi na kumbukumbu za juhudi za Waislam katika kujiletea maendeleo
yao.
Serikali katika kuthamini mchango wa Kleist
katika kupeleka mbele elimu kwa ajili ya watoto wa Kiislam ikamchagua kuwa
katika Provincial Education Committee of Tanganyika Education. Mwanae Abdulwahid na yeye vilevile akaja kuwa
katika Aga Khan Education Committee.
Halikadhalika walimu wawili wa Al Jamiatul
Islamiyya walipewa nafasi muhimu katika siasa na uongozi wa nchi. na Sheikh Juma Mwindadi alifanywa mjumbe katika Baraza la Mji wa Dar es Salaam.
Mwaka 1956 Aga Khan alipotembelea Tanganyika
Waismailia walimnunulia Mercedes Benz 280S yenye usajili DSQ 666 na hii ndiyo
alikuwa akitembeanayo mjini Dar es Salaam.
Mwaka wa 1959 Waismailia
waliamua kuiuza gari hii lakini hawakutaka inunuliwe na Muismailia ila
inunuliwe na mtu yoyote mwenye hadhi katika jamii ya Watanganyika nje yao.
Gari hii aliuziwa Abdul
Sykes na alikaanayo hadi alipofariki 1968.
No comments:
Post a Comment