Dr. Jahazi amefariki mchana huu leo tarehe 13 September, 2017.
Kwake tumetoka na Kwake ni marejeo yetu.
Iko siku mwaka wa 1993 na ulikuwa mwezi wa
Ramadhani nilikuwa nasafIri na ndege ya Air Tanzania Corporation (ATC) kuelekea
Harare kwenye kozi ya Masoko ya Huduma yaani, ‘’Marketing of Services.’’ Wakati
ule nilikuwa nikifanya kazi Bandarini Idara ya Masoko.
Ndege ilikuwa ya alfajir na kwa bahati nzuri Dr.
Jahazi na yeye alikuwa anasafiri na ndege hiyo hiyo kuelekea Harare kwenye
mkutano wa Madaktari. Wakati ule Dr. Jahazi alikuwa akisomesha pale Muhimbili
Faculty of Medicine.
Basi nikamkuta Dr. Jahazi pale uwanjani amesimama
anasubiri ATC wafungue ‘’desk,’’ lao abiria waanze mchakato wa ku -‘’check in,’’
abiria ili wapatiwe, ‘’boarding pass,’’ waelekee, ‘’departure lounge,’’ na
kuingia katika ndege tayari kuwa kuruka.
Dr. Jahazi alikuwa amevaa kanzu nyeupe na
amepiga kilemba cha tabligh.
Ukitamtazama picha ya haraka itakayokujia ni
kuwa huyo ni sheikh wa tabligh siyo Mhadhiri wa Chuo Kikuu.
Siku zile ilikuwa hakuna, ‘’security check,’’
kama hizi za siku hizi za kupitisha watu na mizigo katika, ‘’metal detector,’’ ambazo
kwa sasa ziko kila mahali kuanzia viwanja vya ndege hadi katika mahoteli
makubwa.
Wakati nasalimiana na Dr. Jahazi tukiubiri ATC
wafungue, mara akatokea Balozi Ami Mpungwe wakati ule akifanyakazi Wizara ya
Mambo ya Nchi za Nje kama Balozi na Mkurugenzi wa Afrika na Mashariki ya Kati.
Ami akaja pale tulipokuwa tumesimama na
akatusalimu.
Dr. Jahazi akamuuliza kama na yeye ni msafiri.
Ami akajibu akasema yeye amekuja kuwasindikiza wageni wa serikali na alikuwa
kawaingiza VIP Lounge na alikuwa anaondoka ndipo alipotuona akaona aje
atusalimu.
Dr. Jahazi akamfahamisha Ami kuwa sisi tulikuwa
tunakwenda Harare.
Dr. Jahazi alikuwa mkononi ameshika, ‘’briefcase,’’
na katika ile, ‘’briefcase,’’ alikuwa amefunga kidumu cha lita tano chenye
maji.
Ami akawa kashangazwa na kile kidumu cha maji,
akamuuliza Dr. Jahazi, ‘’Dr. haya maji ya nini?’’
Dr. Jahazi akajibu akasema, ‘’Haya maji natembea
nayo kwa ajili ya kuchukua udhu isije wakati wa sala umeingia na mimi sina maji
ya kutawadha.’’
Jibu lili lilimtosheleza Ami hata na mie pia
kwani nami nilikuwa najiuliza yale maji yalikuwa ya nini ila tu sikupata fahamu
ya kuuliza.
Ndani ya ndege tulikaa pamoja na ilikuwa safari
nzuri sana kwangu.
Dr. Jahazi aliniwaidhi kuhusu utukufu wa Allah
na Mtume Wake na akaniambia kuwa endapo nitaishika kamba ya Allah nitafanikiwa
hapa duniani na akhera.
Siku ile tukiwa angani tukielekea Zimbabwe ndiyo
kwa mara yangu ya kwanza nilipolisikia jina la Prince Badru Kakunguru wa
Uganda.
Dr. Jahazi alipobaini kuwa mimi sikuwa namjua
Prince Badru Kakunguru alianza kunieleza historia ya Uislam Uganda na vipi
Prince Badru Kakunguru alivyofanya juhudi katika kuuepeleka Uislam mbele
Uganda.
Nilishangaa sana kwani sikujua kuwa Dr. Jahazi
juu ya kuwa Bingwa wa Micro Bio-Chemistry Uganga wenyewe alikuwa pia ni mjuzi wa
historia.
Niliona safari ni fupi sana katika ya Dar na
Harare.
Mimi nilikuwa sijafika Harare lakini yeye Dr.
Jahazi alinifahamisha kuwa alikuwa akienda huko mara nyingi kwa shughuli za
mikutano na makangamano ya kitaaluma.
Basi nikamuomba Dr. Jahazi anifahamishe hoteli
nzuri ya mimi kwenda kukaa.
Ilikuwa kozi ya takriban mwezi mzima na nilitaka
nikae mahali pazuri.
Dr. Jahazi alinitazama usoni akaniambia, ‘’Sikiliza
mdogo wangu Mohamed, mimi sikai hoteli, mimi nalala msikitini.’’
Ukweli ni kuwa nilishtuka na kushangaa sana.
Juu ya mshtuko wangu sikusema kitu nilinyamaza
kimya.
Wakati tunatoka nje ya uwanja wa ndege wa Harare
mie nikawa nimemganda Dr. Jahazi niko ubavuni kwake. Mara tu tulipokuwa
tushapita, ‘’Customs,’’ kundi la vijana wa kila rangi nikaona wamemvamia Dr.
Jahazi wakimpokea mizigo yake na kutokana na mazungumzo yao nikajua hawa ni madaktari
wanataaluma wanzake.
Ghafla Dr. Jahazi akawa kageuka si yule
aliyekuwa na mimi ndani ya ndege. Hapa alikuwa Dr. Jahazi ‘’Lecturer,’’ yuko
darasani anasomesha.
Mara atamjibu huyu hiki mara atamjibu huyu kile
kwa Kiingereza kilichonyooka kisawasawa. Hakika wale jamaa ilionyesha walikuwa
wanamuusudu Dr. Jahazi na walikuwa wamengoja kwa hamu.
Yalikuyokuwa yanazunguzwa pale mie sikuambulia
hata moja.
Baada ya kutulia tukaingia katika gari kuelekea
mjini na akanambia kuwa atanipeleka Ambassador Hotel iko katikati ya mji na
akamwambia dereva apite barabara fulani ili anionyeshe msikiti nitakaokuja
kuswali tarweh.
Nakumbuka kichekesho kimoja.
Dr. Jahazi aliposema neno, ‘’mosque,’’ yule
dereva akawa hajui lina maana gani.
Dr. Jahazi alipomfahamisha dereva kuwa ni ‘’msikiti,’’
yule bwana akajibu akasema, ‘’Oh! You mean Muslim church.’’
Dr. Jahazi alikuwa rafiki kipenzi wa kaka yangu
Prof. Mgone toka wote wakiwa wanafunzi pale Muhimbili na nilikuwa nafurahishwa
na kitu kimoja kila tunapokutana.
Ingawa sasa mimi ni mtu mzima lakini yeye
hakuacha kuniangalia mimi kama, ‘’bwana mdogo,’’ wake na katika mazunguzo yetu
siku zote hiki kikijitokeza na mimi nilikuwa siachi kutanguliza, ‘’kaka,’’ kila
ninapozungumza na yeye.
Miezi michache iliyopita tulikuwa sote
tukaachana Msikiti wa Shadhly baada ya kuzungumza njia nzima.
Mwaka wa 2002 Tanzania ilipopitisha Sheria ya Ugaidi,
Dr. Jahazi alivamiwa nyumbani kwake na kutiwa nguvuni kwa kushukiwa kuwa ni
gaidi. Wapelelezi walipekuea nyumba yake chini juu juu chini kutafuta ushahidi
wa ugaidi lakini walichokutananacho katika nyumba na maktaba yake ni mavolumu
na mavolumu ya majarida na mabuku na mabuku ya taaluma yake ya udaktari.
Kosa lake Dr. Jahazi ilikuwa ni yake mapenzi
yake katika dini yake na kuenzi kivazi chake cha kanzu na kilemba hata
anapokuwa darasani Chuo Kikuu Muhimbili akihadhiri.
Allah ampe kaka yangu Dr. Jahazi kauli thabit na
amweke mahali pema peponi.
Amin.
Amin.
No comments:
Post a Comment