Thursday 28 September 2017

KEBEHI KWA MAALIM SEIF MITANDAONI MBONA VYOMBO VYA DOLA VIKO KIMYA?




Utangulizi
Imekuwa jambo la kawaida kwa Maalim Seif kutukanwa a kukebehiwa katika mitandao ya kijamii na watu ambao wanafahamika. Binafsi siku za mwanzo nilijaribu kuwa naandika nasaha kujaribu kuwafahamisha wahusika wa kejeli na matusi kuwa huyu wanaemvunjia heshima ni kiongozi mkubwa katika nchi yetu lakini ilibidi niache kwa kuona kuwa hawakuwa tayari kunisikiliza na zaidi matusi na kejeli zikizidi. Lakini kinachonistaajabisha  vipi vyombo husika kuwa kimya.
MS

Kuna wakati sasa inakaribia miaka 20 watu fulani walinifikiria kuwa nina, ‘’ujuzi,’’ ambao ungekuwa na manufaa katika taifa letu na baadhi ya watu hao ni wakubwa wakataka nikautumie, ‘’ujuzi,’’ huo wangu katika ofisi kubwa sana ya serikali.

Kipindi hiki ni kile kipindi ambacho palikuwa na malalamiko mengi kuwa kuna upogo mkubwa katika kushika madaraka katika serikali kuwa jamii moja fulani imeachiwa kuhodhi serikali nami nilikuwa mmoja wa watu wenye fikra hizo.

Katika walikuwa wametumwa kunishawishi nikubali ombi hili la kwenda kuitumikia serikali yetu ni mwalimu wangu wa Chuo Kikuu ambae yeye tayari alikuwa serikalini na ameshika nafasi kubwa.

Lakini ukweli ni kuwa hii kwangu mie lilikuwa, ombi  la pili, ombi la kwanza lilikuwa niingizwe chamani  kabisa.

Kweli nilistaajabu kwa mtu mdogo kama mie kuonekana kuwa naweza kuwa na manufaa katika utendaji wa ufanisi katika nchi yangu.

Hili pendekezo la utumishi chamani nilimwambia mjumbe na sahib yangu aliyenifuata kuwa akili yangu jinsi ilivyo sitaweza kukamilisha majukumu nitakayopewa kwa ufanisi na kubwa nililohofia ni kuwa vipi nitawatazama ndugu zangu machoni?

Nitaingia msikiti gani kuswali bila kuingiwa na simanzi?
Huu ndiyo ukawa mwisho wa jambo lenyewe.

Hili la pili sikuweza kukataa hapo kwa hapo kwa sababu fulani fulani kwa hiyo nilipeleka hadi CV yangu.

Lakini katika nafsi yangu niliamini kabisa kuwa hili haliwezi kuwa kwani mimi nimefika mbali sana na kukanyaga ardhi ambayo wengi kabla yangu na wajuzi kunishinda hawakuthubutu kutia mguu wao.

Hivyo ndivyo ilivyokuwa baada ya muda siku moja nikapigiwa simu ya dharura nikiendesha gari nikaambiwa haraka nirudi ofisini kwangu nitume tena ile CV yangu mara moja kwani ile ya kwanza haionekani.

Nilitii.

Lakini nilijuwa kuwa hili haliwezekani na kweli hivyo ndivyo ilivyokuwa.
Bahati nzuri au mbaya hata kama yangefanikiwa sidhani kama ningedumu kazini.

Allah hakunijaaliwa ustahamilivu kuacha kusema kile ninachoakiamini kuwa kweli.

Wazee wangu wawili Allah awarehemu, Ally Sykes na Kitwana Kondo wote wakinipenda na wote walipatapo kunambia kwa huruma sana kuwa nitakufa masikini na Mzee Ally alikwenda mbali zaidi alinambia, ‘’Mohamed utakufa masikini kama baba yako Allah kakujaalia vipaji lakini umeshindwa kuvitumia…’’

Bwana Ally alipomaliza kusema maneno haya akaniuliza umri wangu. Nilikuwa na miaka 40.
Ally Sykes akatingisha kichwa kwa masikitiko.

Mzee Kondo yeye alinifananisha na wenzangu wa rika langu na wengine ni marafiki zangu akamwambia mkewe, ‘’Mwanangu huyu ndiye pekee dunia yake haikumkalia vizuri.’’

Nimeleta utangulizi huu kwa kuona imewekwa picha hapa ikimkebehi mmoja wa viongozi wa nchi yetu.

Nimeona na mie nichangie katika hiyo picha lakini kwa kuweka staha kuwa iko siku iliwekwa picha mfano wa hii lakini mimi nilipochangia nikaonywa kuwa nisifanye hivyo nami nikatii na kuomba radhi nikasema kwa kuwa nimeona picha hiyo imewekwa mwekaji na kaandika maneno hakukemewa nikadhani inaruhusiwa.

Mradi kumbe ni makosa naomba radhi mnisamehe.

Sasa katika hili lililo mezani wengi wameona hiyo picha lakini wamekaa kimya kwa nini  mimi?
Lugha ya sasa unaweza kusema kwanini ‘’nimewashwa?’’

Rejea katika utangulizi wangu jibu liko hapo.

Bibi zangu wake zangu mabinti Farijala wakisema, ‘’Masikini mume wetu Mohamed, ule ‘’wazimu,’’ wote wa babu yake Mzee Popo wanae wote umewaruka umekuja kumvaa mjukuu wake.’’

Mie huwaambia watu kuwa Wamanyema wote wewe tuchungiuze tuna wazimu kidogo.
Baba Juma atanisaidia kusadikisha.

No comments: