![]() |
Ali Juma Sleiman |
Wamemuua
mzee wa watu Ali Juma Sleiman bila ya sababu yoyote zaidi tu ya hasad, chuki na
ubaya ulio ndani ya nafsi zao. Mzee huyu ni mtu mzima, kosa lake kubwa ni CUF.
Wamemdhulumu roho yake kwa mateso, uonevu na unyama usiomithilika. Anakwenda
kwa mola wake akiwa na masikitiko ya dhulma si ya mali pekee bali uhai wake,
dhamana yake ya kusimamia famili yake na dhima yake ya kusimama na lililo na
uhalali.
Wamemdhulumu
maisha yake akiwa na majeraha ya vipigo, maumivu ya roho, nafsi na kiwiliwili
kibichi kinachotangulia kwa Muumba wake kwa sababu ya uonevu. Mzee huyu ameacha
famili, leo wanaamka wakiwa na sanda mkononi ya kuenda kumsitiri mzee wao
aliefariki kwa sababu ya dhulma ya wababe dhidi yake na chaguo lake la nani wa
kumuongoza katika utaratibu tuliojipangia.
Mzee
huyu anakoshwa mwili wake, akimwagiwa maji ya kutoka utosini mpaka vidoleni,
bado akivuja damu ya vipigo alivyovipata. Maji yanakosha michibuko ya marungu
aliopigwa miguuni ili anapofika kwa aliemuumba awe msafi, akiyakabili maisha
yake mapya ya akhera kwa sababu ya wababe na dhulma waliomfanyia. Anakafiniwa
na kuvikwa sanda yake, na kusaliwa na jamii ya waislam, masheikh na wanazuoni
ambao kila mmoja anajuwa dhulma iliomfika, dhulma iliopevuka ya kumpotezea
maisha yake.
Tuna
mlolongo wa viongozi wa imani, walioapa kusimama na haki lakini kimnya kwa
unyama unaofanyika. Wameamua kusema na nyoyo zao tu na kuacha nafsi zikielemewa
na ukubwa wa matukio yaliokosa chembe ya uungwana lakini hakuna wa kukemea.
Wanatembea wakitikisa vichwa vyao tu lakini mdomo umebana barabara, hutalisikia
la kupinga dhulma hizi zinazofanyika kula kukicha.
Wamemuua
akiwa na kauli yake, akisimulia yaliomsibu kichwa chini, mtu mzima alievunjiwa
heshima na vijana waliokuzwa katika uislam na waliofunzwa kusimama na wema na
ihsan ambao wengine anaweza hata kuwazaa. Anaondoka duniani akiwa amefunga
macho lakini taswira ya mwisho ya uhai wake ikiwa ni vishindo, khofu, maumivu,
majeraha na istifham ya kuiona roho yake ikimtoka kwa jinsi nguvu kubwa
zilivyotumika kumdhuru na kumdhulumu haki yake ya kuishi.
Wafikirie
watoto wake, mke wake, wajukuu zake, jamaa zake, dada zake na kaka zake.
Wafikirie wale wa karibu watakaoingia kaburini kumsitiri mzee wao wakijuwa kuwa
kilichofanyika dhidi ya mzee wao kimekosa utu na kupitiliza mipaka yote ya
ubinaadam. Ghafla aliekuwa akiitwa baba sasa marehem kwa sababu ya wababe
wanaofugwa wakilishwa na kuvishwa ili kuonea masikini na wanyonge wengine
waliomkataa kiongozi asiewafaa.
Waliokuwa
wakimtegemea wanaamka sio na simanzi za kumpoteza mpendwa wao tu bali mtafaruk
wa mawazo ya maisha baada ya madhila haya yaliopoteza roho ya kipenzi chao.
Anabebwa katika safari yake ya mwisho, huku "Laa Ilaha Illa Llah"
zikisomwa vifuani vya wenye dukuduku la uonevu, wanaotazamana wakifikiri nao
khatima zao dhidi ya madhalimu walio na utayari wa kutoa roho tena kwa ukatili
mkubwa wa vipigo kwa wanyonge wasio na nguvu.
Yaliomfika
huyu mzee ni sehemu ya maisha ya kawaida kwa wapinzani visiwani na bara kwa
sasa. Vipigo kama hivi viko katika kila shehia zetu, na unaweza kukuta kuwa
vimewagusa wazanzibari wengi kutokana na ukaribu wetu. Ukandamizaji unaofanyika
dhidi ya wapinzani hausemeki na leo hii tumempoteza mzee wetu kwa sababu tu ya
ubaya wa wachache waliokosa utu. Wanaojiita waungwana wamebeba kejeli kwa suti
ya rangi ipi na ukubwa gani, huku jahazi wakilitoboa kwa makusudi wakifikiri
litazama upande mmoja tu.
Mwenyezi
Mungu akupokea mzee wetu ukiwa shahid wa kisimama na lililo na uhalali. Akupokee
kwa rehma zake na kukuepusha na kila adhabu huku akikusamehe makosa yako yote.
Uzindukane ukiwa katika utulivu wa nafsi, katika kaburi lako lililojaa nuru na
malaika wema wawe ndio sehemu ya mapokezo yako katika safari yako hii ya
milele.
Mwenyezi
Mungu akujaalie safari hii iwe ni safari ya kheri kwako, ilio na maisha mema
katika pepo yake iliojaa waja wema waliosimama katika ukweli, ihsan na haki.
Mwenyezi Mungu awape subra familia yako na kila alieguswa katika mtihani huu
wenye machungu yasio mithilika.
Allahuma ghfirlahu, warhamhu waskanahu filjana.
Allahuma Ameen.
Allahuma ghfirlahu, warhamhu waskanahu filjana.
Allahuma Ameen.
No comments:
Post a Comment