Friday 29 December 2017

SHEIKH AHMED ISLAM (1930 - 2017) NA MOHAMED SAID


SHEIKH AHMED ISLAM (1930 – 2017)
KIONGOZI SHIRIKA LA UMMA, SHEIKH, BABA WA VIJANA NA MWALIMU

Sheikh Ahmed Islam akiwa Masjid Ngazija akiongoza shughuli

Allah ana njia za ajabu sana za kukutanisha waja wake na kutokana na kusubihana huko mengi yakapatikana. Ilikuwa mwaka wa 1972 niko ndani ya basi la KAMATA (Kampuni ya Mabasi Tanzania) natokea Nairobi likizo. Basi limesimama Korogwe kupakia abiria. Katika basi lile akaingia kijana mtanashati umri wangu karibia miaka 20 akaniuliza kama pale pembeni yangu kiti kile ni wazi ili akae. Nilimfahamisha kuwa kiti ni kitupu. Akakaa na mara akaja mtu mzima dirishani wakawa wanaagana. Yule alikuwa ni baba yake na amemsindikiza. Huyu kijana jina lake ni Charles James Bossa. Bossa kuanzia siku ile ndani ya lile basi akawa rafiki-ndugu hadi hii leo ninavyoandika. Bossa alikuwa amemaliza shule na alikuwa anakwenda Dar es Salaam kufanya ‘’interview,’’ ya kazi Posta. Bossa aliajiriwa na Posta na akafanya kazi hadi alipostaafu miaka michache iliyopita.

Katika taazia hii ya mzee wetu Sheikh Ahmed Islam Bossa amekuwa na msaada mkubwa kwangu kwa kunieleza mengi ya Sheikh Islam kwani alifanyakazi katika Idara ya Rasilimali watu ambayo Sheikh Islam alikuwa mkurugenzi wake na ameshuhudia mengi katika utu, huruma na ukarimu wake kwa wafanyakazi.  Sasa ndiyo nami nakumbuka kuwa katika mazungumzo yetu miaka ile sasa zaidi ya miaka 40, jina la Mzee Ahmed Islam likawa halipungui mdomoni kwake akimtaja kwa sifa nzuri na za kupendeza za ukarimu na huruma kwa vijana waliokuwa katika idara tofauti za shirika lile.  Kabla sijanyanyua kalamu kuandika taazia hii nilimpigia simu Bossa kumpa pole kwa msiba wa mzee wake. Bossa alinistaajabisha kwani alilokujanalo sikuwa nalijua. Baada ya kupokea mkono wangu wa taazia akanambia, ‘’Mimi nilikuwako mazishini na nikamkumbuka na mama yetu kwani hata mama tulimzika katika makaburi yale pale pale tulipomzika Mzee Islam.’’ Nikamuuliza, ‘’Kwani ulikuwa ukimfahamu mkewe? Jibu likaja, ‘’Sana, wakati Mzee Islam alipokuwa mkurugenzi wetu mara kwa mara alikuwa baada ya kazi jioni akituchukua katika gari yake tukienda nyumbani kwake pale Upanga kunywa chai na sambusa, bajia na vitu vingi vya tunu na hapo ndipo tulipojuana na mama. Walikuwa watu karimu mno.’’

Ilibidi nishushe pumzi. Mkurugenzi mzima anajishusha chini kiasi kile cha kuwachukua wafanyakazi walio chini sana kwake kuwaleta nyumbani kunywa nao chai. ‘’Sheikh Islam tukizungumzanae sana na alitusogeza karibu sana na yeye. Sisi alitufanya kama wanae. Hata nakumbuka siku moja katulueleza jinsi alivyonunua ile nyumba yake. Anasema yeye akifanyakazi Cable and Wireless, Zanzibar na baada ya kampuni ile kuvunjwa na kuingizwa katika Shirika la Posta la Afrika ya Mashariki, alipopewa mafao yake yeye alitumia fedha zile kununua nyumba ile Upanga kwa shs: 54,000.00 kwa wakati ule. Sina la kukueleza ndugu yangu Mzee Islam kawanusuru wengi katika kazi. Yeye alikuwa mzito sana wa kuandika barua za karipio kali na kuadhibu. Kawaida yake alikuwa akifanya nasaha na kutoa msamaha kisha akimweleza muhusika njia ya kulipa msamaha ni kwake kuwa mfanyakazi mwema kwa faida yake mwenyewe na familia yake na kwa shirika na nchi iliyompa fursa ya kazi ili aendeshe maisha yake bila tabu.’’

Nilikuwa kimya siwezi hata kutia neno ila kumuitika rafiki yangu Bossa ili ajue simu haija katika na mimi namsikiliza kwa makini. ‘’Mzee Islam alikuwa kama mlezi wetu, baba yetu akiuzuia mkono wake kuadhibu. Kuna mwenzetu alikuwa afukuzwe kazi kama si Mzee Islam kumsaidia kisha kumkalisha kitako. Ile kesi ilikuwa ya mtu kupewa ‘’summary dismissal,'' na yeye alilijua hilo kwani aliondoka kazini akabaki nyumbani kusubiri kufukuzwa kazi.’’ Mzee Islam aliagiza aitwe aje kazini. Mzee Islam alimsamehe baada ya kumpa nasaha. Huyu jamaa hivi sasa amestaafu kwa salama akiwa mfanyakazi wa Shirika la Posta. Haya yalinitosha sikua na haja ya zaidi. Maisha yake mwenyewe Sheikh Islam yalikuwa mfano tosha kwa wale aliokuwa akiwaongoza. Hakuna haja ya kumfananisha na wakurugenzi wengi tuliopata kuwajua na pengine kufanyanao kazi kwani hawastahili wala hawana hadhi hata ya kuwekwa kwenye mizani moja na Sheikh Islam.


Wafanyakazi mafundi wa mawasiliano ya simu kutoka Shirika la Posta Tanzania
waliopelekwa Zimbabwe kwa juhudi za Sheikh Ahmed Islam wakiwa na Mwandishi
(aliyevaa miwani) mjini Harare March 1993


Baada ya Cable & Wireless kampuni ya Uingereza kufunga shughuli zake ndiyo ikawa Extelcomms chini ya Jumuiya ya Afrika ya Mashariki na ilipovunjika jumuia Extelcomms ikaunganishwa na Posta na kuwa Tanzania Posts & Telecommunications Corporation. Mwaka wa 1993 zikagawanyika kuwa   TTCL na TPC. Jumuia ya Afrika ya Mashariki ilipovunjika mwaka wa 1977 Sheikh Islam akiwa Mkurugenzi wa Rasilimali Watu Posta alifanya kazi kubwa ya kuwakaribisha nyumbani wafanyakazi wa iliyokuwa East African Posts and Telecommunication wengi wao wakiwa wafanyakazi waliokuwa wakifanya kazi Kenya na Uganda. Hawa walirudi nyumbani wakiwa na hofu kubwa ya hali yao ya baadae nchini Tanzania. Huu ulikuwa wakati hali ya uchumi Tanzania ilikuwa ngumu sana. Sheikh Islam aliwatia moyo na kuwatuliza akiwaambia hakuna shida ya kudumu daima. Zimbabwe ilipopata uhuru wake mwaka wa 1980 Wazungu waliondoka kwa wingi na pakawa na shida ya wataalamu wa simu nchini. Sheikh Islam alisaidia sana akishirikiana na serikali katika katika kuchagua mafundi wa simu ambao walikwenda Zimbabwe kusaidia kuweka mambo ya mawasiliano sawa. Mafundi hawa kutoka Tanzania wengine wao wakiwa bado vijana wadogo baadae walihamia Botswana na nchi nyingine za Kusini ya Afrika katika kutafuta maslahi zaidi. Katika vijana waliopelekwa Zimbabwe na Sheikh Islam ni rafiki yangu Erick Mpwagi ambae baadae alihamia Marekani.

Mimi binafsi kumbukumbu yangu ambayo itabaki katika fikra yangu ni uradi wa kila Alkhamis Msikiti Ngazija ambapo yeye na Sheikh Aboud Maalim walikuwa hawakosi na kwa hakika ndiyo waliokuwa wakituongoza. Kadri ya kukumbuka kwangu huu uradi umekuwa ukisomwa hapo msikitini miaka na miaka na uliwakutanisha vijana na wazee hapo msikitini kutoka sehemu tofauti za mji wa Dar es Salaam. Uradi huu mbali ya kumtukuza Allah, ulikuwa sababu kubwa ya kujenga udugu na mapenzi baina ya wengi kwani nawafahamu hii leo watu ambao nisingefahamiana kwa kiasi cha undani huu uliopo baina yetu kama si ule uradi. Kwa hakika kwa sisi ambao wakati ule tulikuwa vijana sana si jelebi, kababu na samabusa ndizo zilizokuwa zikitupeleka katika uradi, hapana. Uradi ule ulitunufaisha zaidi ya hapo. Labda kama si uaradi huu wengi tusingeingiliana na Sheikh Islam na watu wengine kwa kiasi cha kuwa na mapenzi ya kiasi kilichokuja kujengeka.

Nafasi yangu kubwa ya kumjua Sheikh Islam kwa karibu zaidi ilikuja mwaka 1997 tulipokwenda sote Umrah na ndege ya kwanza ya Shirikia la Ndege la Tanzania ilipofanya safari yake ya kwanza kwenda Jeddah, Saudi Arabia. Namshukuru Allah kuwa si tu kuwa nilipata kuwa karibu yake tukiwa safarini, bali tulikuwa sote katika dhifa tuliyoandaliwa Al Harithy Hotel, moja ya hoteli mashuhuri Jeddah na vilevile mimi na Dr. Dau tulilala ubavuni kwake katika nyumba ya Tanzania Haj Trust ambako baadhi yetu tulifikia. Si haya tu bali Sheikh Islam alituongoza Makka katika Umrah na baada ya kumaliza alisimama mbele ya Kaaba akaomba dua hadi machozi yakammwagika. Sote tuna machozi lakini tabu kutoka kwa ugumu wa nyoyo zetu.

Kulia Sheikh Ahmed Islam, Dr. Ramadhani Dau na Mohamed Said, Minna
Safari ya Umrah 1997

Baada ya kufanya Umrah baadhi yetu tulikwenda Madina kumzuru Mtume SAW Sheikh Islam akituongoza. Nakumbuka tukiwa Madina asubuhi baada ya kusali Fajri Masjid Nabawy Sheikh Islam, Balozi Ramadhani Dau na mimi tulikwenda nje si mbali na msikiti kulikuwa na kiosi kinauza chai ya mkono mmoja. Basi wakati tunakunywa chai sikumbuki nani alianza kusoma kasda maarufu, ‘’Twala Al Badru,’’ ninachokumbuka ni kuwa asubuhi ile ilikuwa njema sana kwangu mimi na Dr. Dau kwani Sheikh Islam na  yule mwenye kile kibanda wakawa kama vile wako kwenye ‘’duet,’’ wanapokezana kusoma, mmoja akimaliza ubeti mwenzake anapokea. Walipomaliza kasda hii wakaingia katika kasda nyingine, ‘’Yarabibi Mustafa…’’ Binafsi kasda hizi zilinikumbusha mbali sana Moshi kwa Mwalimu Juma aliyekuwa akitusomesha watoto Qur’an Msikiti wa Ijumaa, Mtaa Chini. Miaka mingi sana sasa nikiwa mtu mzima nilionana na Maalim Juma pale pale msikitini na nyuma tu ya pale walipokaa ndipo aliponishikisha alif kwa kijiti. Maalim Juma alikuwa amekaa na wazee wenzake. Maalim Juma hakunikumbuka kwani ilikuwa zaidi ya miaka 40 imepita. Mwenzake mmoja anaenifahamu akamwambia, ‘’Sheikh Juma lisikutishe lile gari lake pale huyu mtoto umemsomesha hapa.’’ Nikizisikiliza hizi kasida mbele ya Msikiti wa Mtume SAW nilikuwakumbuka waalimu wangu wote, Maalim Badi na Maalim Mussa wote weshatangulia mbele ya haki.

Sheikh Islam katika utu uzima wake akiwa kachoka na anatembea kwa shida hakuacha kuhudhuria shughuli zote alizokuwa akishiriki wakati ana nguvu zake. Sasa ndiyo naanza kuelewa kwa nini kila alipokuwa kakaa na nalitumia neno hilo kwa maana yake halisi. Sheikh Islam alikuwa akija mazikoni Makaburi ya Kisutu atakaa kwenye mabenchi yale ya saruji pale karibu na lango la kuingilia. Hapo atakuwa anapokea mikono ya wakubwa na wadogo wanaokuja kumlaki. Hali ni hivyo hivyo akiwa kakaa kwenye kiti chake upande wa kulia Msikiti wa Maamur. Kila aingiae atakwenda kumsalimu Sheikh Islam kiasi mimi wakati mwingine nikimuonea tabu kuwa mbona hawa watu hawamwachi Sheikh Islam akapumzika kila dakika kafika mtu. Lakini hii ndiyo ilikuwa namna ya watu kuonyesha heshima na mapenzi yao kwake. Sheikh Islam alibeba mambo mengi ya watu mabegani kwake bila kuona wala kuhisi tabu.

Kama alivyowalea wafanyakazi chini yake aliokuwa akiwaongoza wengi wao vijana wa kike na wa kiume hivyo hivyo ndivyo alivyowalea vijana katika jamii. Sheikh Islam katatua migogoro mingi ya kifamilia na kasaidia vijana wengi kupata kazi na wengine kusoma ndani na nje ya nchi na wengine kuoa na kuolewa. Hapa nitakielza kisa kimoja. Kisa cha mwenzetu mmoja ambae alitaka kuposa katika moja ya koo za Dar es Salaam lakini palikuwa na vikwazo kadhaa ambavyo vilikuwa kwanza viondolewe na wazazi wa pande zote mbili ili posa ipelekwe na baadae wazee watoe idhini ya ndoa. Hofu ilikuwa ni wapi mambo yaanze na ugumu ulikuwa hapo kuwa jambo lenyewe likikosewa kwenye hatua za awali huenda likavurugika kabisa. Kwa kawaida wazazi wa binti huwa hawataki kabisa kuonyesha kuwa wao ni wahitaji wa mtoto wao kupata mume. Kwa ajili hii husubiri wafatwe kwa taadhima zote zikiwa zimezingatiwa. Ndugu yangu alikuwa amezama kwenye lindi la mapenzi hajui afanye nini avuke kizingiti kilichokuwapo.

Sote tukimjua Sheikh Islam heshima yake katika familia zetu. Wazee wetu wakimuheshimu Sheikh Islam mwisho wa staha. Huyu ndugu yangu akaenda kwa Sheikh Islam nyumbani kwake kueleza kuwa anataka kuoa lakini pana ugumu. Nilivyokuwa namfahamu Sheikh Islam sina wasiwasi wowote kuwa ndugu yangu kwanza alipokelewa kwa utulivu wa hali ya juu na akamsikiliza na kumuuliza maswali khasa kutaka kuipata yakini ya jambo lenyewe. Ndugu yangu yeye alikuwa kaweka uzito juu ya kuwa wazazi wa pande zote mbili wamekuwa wagumu. Sheikh Islam yeye akawa anamtuliza kwa kumwambia kuwa jambo la ibada haliwezi kuwa gumu kwa yeyote amuogopae Allah labda kama halitofanikiwa ni kwa qadar ya Allah mwenyewe hataki.

Sheikh Islam alikuwa anajua kuziweka heshima za watu na alikuwa mtu wa kujishusha sana hakuwa yule mtu wa makuu wa kunyanyua simu akazungumza na mtu kwa mbali. Baba wa Bwana Harusi mtarajiwa alipofatwa juu na mama kuambiwa kuwa Sheikh Islam amekuja yuko chini alishtuka. Mzee, baba wa Bwana Harusi mtarajiwa alishtuka. Sheikh Islam kugonga mlango wa nyumba yoyote Dar es Salaam kuja kuwaona wenye nyumba ile ni heshima ya pekee isiyo kifani. Huyu ni mcha Mungu mtu muungwana, kipenzi cha watu. Haraka mzee kashuka chini akiziruka ngazi mbili mbili tayari tabasamu kubwa limetanda uso mzima kumlaki Sheikh Islam. Baada ya kumkaribisha na kukaa na kahawa kuwekwa wakawa wanaulizana hali. Huyu mzee wetu mtu mkubwa sana na Maa Shaa Allah ni mtu wa kujiweza sana lakini yeye alikuwa anajua ndani ya dhati ya nafsi yake kuwa nyumba yake Allah kaikumbuka kwa kumleta Sheikh Ahmed Islam. Hili kwake ilikuwa ni baraka kubwa isiyo na mfano.

Sheikh Islam alianza mazungumzo kwa kusoma aya ya Qur’an mnasaba na lile aliloendea. Kisha akamgusia vipi wazazi wanakasirishwa na watoto kiasi watoto wanakuwa na uoga hata wa kuwaendea wazazi wao. Akamwambia mzee wetu, ‘’Mtoto kaja kwangu kwa kuwa ana hofu kubwa ndani ya nafsi yake juu ya Allah na wewe baba yake. Anajua kuwa bila ya radhi yenu yeye hana kitu mbele ya Allah. Apate radhi yenu nyinyi wazazi wake ndipo yeye atakuwa na mafanikio hapa duniani na kesho akhera.’’ Sheikh Islam alikuwa mtu fasaha sana labda kwa ile hifdh yake kubwa ya Qur’an na nyuradi chungu mzima. Kufika hapo akataka kujua tatizo nini kiasi posa isipelekwe nyumba ile na kijana wao akaoa. Sheikh Ahmed Islam akaelezwa na bahati nzuri maelezo ya mzee yalikuwa sawasawa na yale aliyopewa na Bwana Harusi mtarajiwa. Kikao kikamalizwa kwa mzee kumshukuru sana Sheikh Islam na kumwambia kuwa wao hawatakuwa na pingamizi madam yeye analisimamia jambo lile.

Mimi ni mmoja wa walioshudia harusi nyumbani kwa Bi. Harusi, Sheikh Islam akiwa kakaa ubavu kwa ubavu na baba wa Bwana Harusi. Bwana Harusi alikuwa kapendeza, sura inang’ara kwa tabasamu na furaha. Ndoa hii imetoa mtoto ambae hiVi sasa kila siku baada ya kutoka shule anachukua mfuko wake ambao ndani kuna juzuu yake anakwenda kusoma Qur’an chuo cha jirani na nyumbani kwao. Kila siku ya Eid huyu mtoto na baba yake wanakuja kusali Eid Maamur na baada ya sala watapita kwa Sheikh Ahmed Islam kumwamkia. Mtoto akiwa hajui kama si juhudi za huyu mzee aliye mbele yake labda asingelizaliwa na baba yake huyu.  Huu ni mfano mmoja katika mingi kwa yake aliyofanya marehemu Sheikh Islam.  Katika uhai wake Sheikh Islam wanasema waliokuwa karibu yake kuwa alipeleka posa 200 na zote zilikubaliwa isipokuwa moja. Rafiki yangu Charles James Bossa anasema Sheikh Islam hakuacha kumshinikiza kufunga ndoa hadi alipooa. Kwa maneno yake anasema, ‘’Mzee Islam kwetu sisi tuliokuwa tukifanyakazi Posta alikuwa baba na rafiki. Huenda ni haya malezi ya Sheikh Islam kuwa sababu ya rafiki yangu kwenda kusoma Chuo Cha Mzumbe na kisha kupata mafunzo zaidi Uingereza.  


Kulia: Sheikh Ahmed Islam, Sheikh Ali Hassan Mwinyi, Sheikh Aboud Maalim,
Himid Ashraf na Said Kassim

Hakika ni tabu sana kumwandika Sheikh Ahmed Islam bila ya kumtaja rafiki yake kipenzi Sheikh Aboud Maalim. Wawili hawa walikuwa mithili ya ambari na zinduna. Muda mwingi sana walikuwa pamoja na walifanya mengi katika kuusukuma mbele Uislam. Kama alivyokuwa Sheikh Islam, Sheikh Aboud Maalim alikuwa mzee wangu na mtu wangu wa karibu. Inawezekana pengine bila ya wao wenyewe kufahamu, mapenzi baina yao na mapenzi yao kwa watu wengine walijenga kundi kubwa la watu ambao wote kwa umoja wao wakiwapenda na kuwaangalia kama viongozi katika jamii. Nakumbuka mmoja katika watu ambao walikuwa katika kundi hili ni marehemu Kiaratu Hussein. Sheikh Islam alipofiwa na mkewe msiba ule uliwapiga wengi waliokuwa karibu na yeye na Kiaratu aliathirika sana. Tukawa tukizungumza ananifahamisha vipi Sheikh Islam alivyokuwa mwenye huzuni kwa msiba ule na namna gani Sheikh Aboud Maalim alivyokuwa akimfariji kila alipokuwa kamuona kakaa msikitini kajiinamia. Kiaratu akiniambia kuwa kuwa Sheikh Aboud alikuwa akimshika akimpigapiga na kumwambia, ‘’Ahmed stahamilili mshukuru Allah…’’ Hawa walikuwa watu waliopendana kwa ajili ya Allah na kwangu mimi nilijifunza kitu kingine kuwa watu wema, wema wao huambukiza wale waliowazunguka hadi watoto wadogo.

Kiaratu alikuwa na mwanae akiitwa Hussein. Miaka ile alikuwa mtoto mdogo wa shule ya msingi na kila mwezi wa Ramadhani alikuwa akifuatana na baba yake pale msikitini Maamur. Kiaratu yeye ndiye alikuwa akituongoza kwenye Sala ya Tarweh kwa nyuradi na kwa hakika Tarweh ya Maamur ilikuwa ikipendeza. Mwanae Kiaratu Hussein nikimuona akiswali safu za nyuma na watoto wenzake kati yao ni Mohamed Bakashmar mtoto wa Ahmed Rashad na Mohamed mwingine mtoto wa Dr. Amza Mahunda. Hawa watoto wote walikuwa wakija pale msikitini wamefuatana na baba zao. Baada ya sala hawa watoto watakwenda kumwamkia Sheikh Islam na yeye atawashika mikono na kichwa bila shaka akiwaombea dua. Miaka ikaenda na Kiaratu akatangulia mbele ya haki. Ramadhani ilipofika nikawa naiambia nafsi yangu kuwa Ramadhani hii Tarweh itapooza bila ya sauti ya Kiaratu pale mbele. Nilipata mshtuko mkubwa sana usio na kifani. Mara baada ya kumaliza Sala ya Isha na suna nikamuona Hussein, mtoto wa Kiaratu kanyanyuka kasimama mbele ameikabili kibla analeta nyuradi alizokuwa anasoma marehemu baba yake. Kilichotufurahisha wengi naamini si tu kumuona mtoto kashika nafasi ya baba yake katika jambo kubwa la ibada bali na kule pia alivyoshabihiana na baba yake kwa sauti na zile ‘’gestures,’’ alipokuwa anasoma. Safu ya mbele pale namuona kasimama Sheikh Islam na safu yake maarufu iliyozoeleka pale Maamur. Nikaiuliza nafsi yangu, ‘’Huyu Hussein, huyu mtoto lini kapewa haya mafunzo? Sikutaabika sana kuona ushawishi wa Sheikh Islam na dua zake kwa hawa watoto waliokuwa wakisali pale na baba zao.

Kipo kisa kingine cha Mohamed mtoto wa Ahmed Rashad. Kama mwenzake siku zote alikuwa kwenye jicho la Sheikh Islam pale msikitini. Siku moja Sheikh Islam alikuwa anasafiri na kulikuwa na uradi ukisomwa pale msikitini katika baadhi ya siku. Sheikh Islam akamwambia Mohamed kuwa yeye atakuwa anaongoza kusoma uradi ule hadi yeye atakaporejea. Akamkabidhi Mohamed kitabu cha uradi ule. Mohamed aliongoza uradi ule hadi siku Sheikh Islam aliporudi. Aliporudi ilipofika wakati wa uradi ule Mohamed akampa kitabu Sheikh Islam na yeye akawa kimya. Sheikh Islam akamwambia Mohamed aendelee kusoma uradi ule. Bila kufungua kitabu Mohamed akaanza kusoma ule uradi ghibu. Baba yake Ahmed Rashad na Sheikh Ahmed Islam wanamtazama na kumsikiliza. Nitahitimisha kipande hiki kwa kumweleza Mohamed mwingie, mtoto wa Dr.Mahunda. Katika maziko ya Sheikh Islam nikamuuliza Dr. Mahunda Mohamed yuko wapi nilikuwa sijamuona muda. Dr. Mahunda akanambia baada ya kumaliza chuo kikuu Uingereza Mohamed kenda India kusoma shahada ya pili.

Haya ndiyo matunda ya Sheikh Islam na ndiyo wanafunzi wake ambao ambao nimewaona kwa macho yangu mwenyewe akiwalea pale msikitini wakiwa watoto wadogo wakiswali safu za watoto nyuma ya msikiti wakati wakubwa wanasali. Leo ni vijana wakubwa na ndiyo hawa nawaandika hapa. Hussein Kiaratu yuko Uingereza anasoma, Mohamed Bakashmar, mtoto wa Ahmed Rashad ni Ph D Political Science anafundisha katika moja ya vyuo vikuu Malaysia na kaoa Mmalay na ana watoto na Mohamed Mahunda yuko India In Shaa Allah anafanya shahada ya pili. Haya ndiyo matunda ya uongozi wa Sheikh Islam. Hakuwa mfano kwa vijana peke yao bali hata kwa watoto wadogo ambao kwa wakati ule walipokuwa wadogo huenda baadhi yetu walipochokozana safu za nyuma wakati tunasali walitukera. Lakini babu yao Sheikh Ahmed Islam baada ya sala akiwashika vichwa na kuwaombea dua Allah awaongoze watie furaha kwenye nyoyo za wazazi wao na ndani ya nyoyo za umma.

Hatutaweza kummaliza Sheikh Ahmed Islam. Sheikh Islam alikuwa mtu wa pekee. Tunaomba Allah amsamehe dhabi zake na amweke mahali pema peponi.
Amin.

No comments: