TUNAYOJIFUNZA
KUTOKA KWA SHEIKH AHMED ISLAM
Kufuatia msiba wa mzee wetu
Sheikh Ahmed Islam, niliandika taazia kuelezea wasifu wake na mchango mkubwa
alioutoa kuwaendeleza Waislamu na hasa kazi kubwa aliyoifanya kuwainua viijana
wa Kiislamu kielimu. Baada ya kuandika taazia hiyo, nimekuwa nikipokea maoni
mengi sana kutoka watu mbalimbali ndani na nje ya nchi. Wengi wao wametoa
ushuhuda wa namna ambavyo wao binafsi walivyosaidiwa na marehemu Mzee Islam.
Wengi zaidi wameonesha hamasa ya kutaka kuiga mfano wa Mzee Islam japo kwa
uchache.
Kama nilivyoandika kwenye
taazia, kifo ni faradhi na kila mmoja wetu ataonja umauti. Mzee Islam
amekamilisha faradhi hii. Lakini pamoja na kuondoka kwake, ametuachia darsa na
changamoto kubwa. Yapo mengi sana ya kujifunza kutoka kwake. Kutokana na umri
tuliokuwa nao, ni dhahiri kuwa baadhi yetu hatutoweza kudumisha sunna ya
kufunga Jumatatu na Alhamisi na kuanza kuswali Tahajud kwa zaidi ya miaka 60
kama alivyofanya Mzee Islam kwa sababu umri umeshatutupa mkono. Lakini hata kwa
upande wa vijana, ni dhahiri pia kutokana na harakati za kupambana na maisha,
wengi wao wataona ni uzito mkubwa kufanya hivyo kwa muda wa uhai wao, japo
hawajui urefu wa muda uliobaki.
Kama nilivyosema awali,
marehemu Mzee Islam amefanya mengi na yapo mambo mengi ya kumuiga kila mtu kwa
nafasi yake. Iwapo hayo ya kufunga Jumatatu, Alhamisi na kuswali Tahajud
hatuyawezi, basi hakuna hata jema moja la marehemu Mzee Islam ambalo tunaweza
kuiga na kulidumisha? Kwa mfano, kwa kuwa Mzee Islam ametumia muda mwingi wa
uhai wake kusaidia vijana wa Kiislamu kupata elimu, hivi sisi tuliobaki (na
hasa wale walionufaika na juhudi zake) hatuwezi kuanzisha taasisi (Ahmed Islam
Foundation? --- AHIFO) na kujilazimisha kuchangia angalau shs. 10,000.00 kwa
mwezi (au zaidi kulingana na uwezo wa mtu) kwa ajili ya kusaidia kusomesha
mayatima au wanafunzi wasio na uwezo? Kuna njia bora ya kumuenzi Mzee Islam
zaidi ya kudumisha mambo ambayo ameyasimamia?
Iwapo watapatikana watu 1,000
ambao watachangia shs. 10,000.00 kwa mwezi, taasisi itakusanya shs. 120 million
kwa mwaka, fedha ambazo zinaweza kusomesha wanafunzi zaidi 100 kwa mwaka kwa
kiwango cha Chuo Kikuu. Najua wapo watakaosema kuwa uzoefu unaonesha kuwa
taasisi zilizoanzishwa kwa utaratibu kama huu wa kuenzi mazuri yaliyoachwa na
marehemu hazikuwa na mafanikio. Mfano ni Sheikh Kassim Juma Foundation,
Abubakar Tambaza Foundation nk. Kwa upande mmoja kuna ukweli kwenye kauli hii.
Lakini zipo taasisi ambazo zilianzishwa kwa malengo kama haya na zimepata
mafanikio makubwa sana. Mfano mzuri ni Hassan Maajar Trust.
Hii ni taasisi ambayo
ilianzishwa tarehe 11 Julai 2011 kufuatia kifo cha ajali ya gari cha kijana
Hassan Majaar kilichotokea tarehe 11 Novemba 2006 Mbabane Swaziland. Wakati wa
kifo chake, Hassan alikuwa na miaka 18 na alikuwa anapenda sana kufundisha
michezo mashuleni kwa vijana wasiojiweza. Kutokana na sababu hiyo, wazazi
wake waliamua kuanzisha taasisi ya kufadhili madawati, vitabu, kompyuta nk.
Hadi sasa Taasisi ya Hassan Maajar imeshanunua na kusambaza madawati zaidi ya
9,000 kwa ajili ya wanafunzi zaidi ya 30,000 kwenye mikoa 10. Lengo lao ni
kununua madawati 3 milioni. Iwapo familia ya Bibi na Bwana Maajar
wameweza kufanya mambo makubwa kama haya tena kwa muda mfupi, naamini kabisa
familia ya Mzee Islam ambayo inajumuisha wale wote walionufaika na jitihada
zake wanaweza kufanya mambo makubwa zaidi.
Wengi walioguswa na taazia
wamenitumia ujumbe wa simu kuonesha hamasa zao na kusema wanatamani wafanye
angalau 10% ya aliyoyafanya Mzee Islam. Hii ni ishara nzuri. Lakini hamasa
na kutamani peke yake havitoshi. Wakati umefika tuzibadilishe hamasa zetu ziwe
ni vitendo. Marehemu Mzee Ahmed Islam alikuwa anaswali Tahajud kila siku
kwa zaidi ya miaka 60. Alikuwa anafunga mara mbili kila wiki kwa zaidi
ya miaka 60. Kwa sababu mbalimbali nilizozieleza hapo juu inaelekea wengi wetu
hatuwezi kufikia daraja hiyo. Lakini hivi kweli wengi wetu hatuwezi kuchangia
shs. 10,000.00 kwa mwezi? (si kwa kila siku au kila wiki
kama alivyokuwa akifanya Mzee Islam).
Nawaomba wale wote walioguswa
na taazia hii, waweke nia na wawe tayari kuchangia angalau shs 10,000.00 kwa
mwezi ili kuendeleza mazuri aliyoyasimamia mzee wetu Ahmed Islam wakati wote wa
uhai wake. Ili kulipa msukumo jambo hili, namwomba Mhe Dr. Hussein Mwinyi
kwa upande wa wanaume na Dr. Mashavu kwa upande wa wanawake washirikiane na
watoto wa Mzee Islam katika kulianzisha na kulisimamia jambo hili jema. Hii
itakuwa ni sadaqa nzuri ya kumtolea mzee wetu. Kwa upande mwingine kuanzishwa
kwa taasisi hii kutatoa fursa kwa watu wengi kupata fadhila za kusaidia
mayatima na masikini.
No comments:
Post a Comment