Friday 22 December 2017

VITABU NILIVYOSOMA MWAKA 2017 NA ZITTO KABWE


Utangulizi

Mh. Zitto Kabwe

Mh. Zitto Kabwe ndiyo sasa nimejua kuwa ni mgonjwa na anahitaji kuaguliwa ila maradhi yanayomsibu ni maradhi mazuri kila mtu amuombe Mola amjaalie na sababu ni kuwa kwa kawaida maradhi hufifilisha mwili lakini maradhi haya badala ya kuchosha mwili hayo huujenga mwili ukawa imara na siha nzuri hasa ubongo. Mh. Zitto ni msomaji wa vitabu wa sifa. Mwaka jana aliweka orodha ya vitabu alivyosoma mwaka mzima. Nilimuonea wivu sana lakini ni ule wivu mzuri wa mimi kutamani niwe kama yeye si ule wa hasad wa kutaka neema ile ya usomaji imuodokee hata kama mimi sitoipata. Hii ni roho mbaya.

Leo mmoja wa marafiki wa Mh. Zitto kwa kuwa anajua mimi ni mpenzi wa vitabu ingawa si msomaji wa kiwango cha Mh. Zitto kanirushia makala aliyoandika Mh. Zitto (ambayo ndiyo hiyo hapo chini) kunionyesha orodha ya vitabu alilvyosoma rafiki yetu katika miezi kumi na mbili iliyopita. Nimeogopa sana nikajiambia huyu Zitto ni ‘’Jamal al Layl,’’ mkeshaji, akisoma usiku kutafuta elimu. Hii imenifanya nielewe kwa nini Bunge hukaa wima, likasimama na kutulia tuli kama maji mtungini wakati Mh. Zitto anachangia hoja yoyote Bungeni. Hakika akili mtu huzaliwanazo lakini kusoma kunaongeza sana maarifa.

Nimemtia Mh. Zitto katika orodha yangu ya watu nikiwausudu sana miaka na miaka kwa ajili ya maktaba zao na mapenzi yao ya vitabu na nitawataja lau si kwa mpangilio wa uzito wao. Naijua Maktaba ya Abdilatif Abdallah maktaba yake nimeiona London na Humburg, Mashaallah siwezi kuihadithia yataka mtu aishuhudie kwa jicho lake mwenyewe. Naijua maktaba ya Juma Mwapachu ingawa miaka mingi sijaoina na ya Walter Bgoya. Ukifika nyumbani kwa watu hawa unaweza kuonekana huna adabu jinsi utakavyokuwa unachakura vitabu safu na safu ukutani badala ya kutulia kweye kochi kama mgeni na hutoweza kuvimaliza vitabu hivi.

Napenda kuhitimisha kwa kusema kuwa zamani kidogo Juma Mwapachu alipata kuniambia kuwa Maktaba ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere iliyoko Butiama ni ya kipekee. Itapendeza sana kama waheshimiwa wetu In Shaa Allah na wao watapata ugonjwa huu wa kupenda kusoma kama Mh. Zitto Kabwe Mbunge wa Kigoma, Mjini.
MS
Vitabu Nilivyosoma Mwaka 2017
Zitto Kabwe



Niliuanza mwaka kwa matumaini makubwa kuhusu usomaji wa vitabu. Mwezi februari Prof. Karim Hirji alinipa zawadi ya vitabu 11 na mimi mwenyewe nilinunua vitabu 12, lakini sikuweza kusoma vyote kutokana na ama kununua vitabu vipya kila ninaposafiri ama kuingiliwa na shuguli nyengine. Mwaka 2017 nimesoma vitabu 36 tu na vitabu viwili navisoma kwa pamoja kumalizia mwaka.

Wakati mwaka 2016 nilisoma vitabu vingi kuhusu udikteta na hususan namna udikteta mamboleo unavyotekelezwa nchini Urusi mwaka huu nilijikita sana katika kupanua wigo wa uelewa kuhusu itikadi ya Ujamaa. Kwamba mwaka 2017 ni miaka 50 ya Azimio la Arusha kulichangia sana kutoka vitabu vingi vinavyohusu Ujamaa au Wajamaa.

Mwaka 2016 nilisoma riwaya nyingi kuliko mwaka huu ingawa nimeendelea na kazi za Mankel na Grisham, pia nimesoma kazi za Ally Saleh ( moja nimeorodhesha na nyengine sijaorodhesha maana bado najisomea au nazirudia kuelewa muktadha wake).

Orodha yangu ya mwaka huu ni hii pamoja na maelezo kidogo.

Mwanasiasa Mjamaa wa Uingereza Jeremy Corbyn alinivutia mno mwaka 2017 na kuanza kusoma vitabu vilivyomwandika ili kumwelewa zaidi na kuelewa namna alivyofanikiwa kukichukua na kukiongoza Chama cha Labour cha Uingereza. Nilibahatika kukutana naye na tangu mwezi Februari amekuwa ni rafiki mkubwa sana. Kuwa na Mjamaa kama Kiongozi wa Chama Kikuu cha Upinzani kwenye nchi ya Magharibi, nchi ya G8 ni jambo kushangaza kidogo kwa dunia ya sasa ambayo kuna watu wanamini kuwa Ujamaa hauna nafasi tena. Nilimsoma sana Corbyn na pia Mjamaa mwengine Bernie Sanders wa Marekani. Hii ilinifanya nisome kitabu kingine kuhusu namna siasa zinavyobadilika kabisa katika nchi za Magharibi na kupelekea watu wenye misimamo mikali ya kulia na kushoto kuibuka. Emanuel Macron ambaye sasa ni Rais wa Ufaransa alishangaza dunia mwaka 2017. Hilo ndio kundi la vitabu 6 vya vyanzo.

1. Jeremy Corbyn: Accidental Hero
W Stephen Gilbert

2. The Candidate: Jeremy Corbyn’s improbable path to power
Alex Nunns

3. Corbyn: The strange rebirth of radical politics
Richard Seymour

4. Our Revolution
Bernie Sanders

5. The rise of the Outsiders: How mainstream politics lost its way
Steve Richards

6. The French exception: Emmanuel Macron-the estra ordinary rise and risk
Adam Plowright

Mwaka 2017 nilitumia muda mwingi kuelewa vizuri itikadi ninayoamini ya Ujamaa. Hivyo nilisoma vitabu kuhusu baadhi ya watu walioandika kuhusu au kujenga Ujamaa nyakati mbalimbali na sehemu mbalibali za dunia. Vitabu 10 vifuatavyo vinahusu Ujamaa na wajamaa. Katika kundi hili napendekeza kitabu cha Yanis Varoufakis kuhusu historia ya ubepari kwa watu wanaotaka kuelewa mfumo wa uchumi wa soko unavyofanya kazi.

7. Rosa Luxembourg or: The Price of Freedom

Jorn Schuetrumpf
8. My Life

Fidel Castro with Ignacio Ramonet
9. October: The story of the Russian Revolution

China Mieville
10. Marx’s Capital

Ben Fine and Alfredo Saad-Filho
11. 75 Years of the Communist Party of Vietnam

12. Liberalism and its discontents: Social Movements in West Africa b
Ndongo Samba (Ed)

13. Talking to my daughter about Economy: A brief history of capitalism
Yanis Varoufakis

14. The enduring relevance of How Europe Underdeveloped Africa
Karim Hirji

15. The contradictions of Capital in the Twenty-First Century
Jeremy S and Nicole R

16. Social Security works
Nancy Altman and Eric Kingson

17. 23 Things They Don’t Tell You about Capitalism
Ha-Joon Chang

Afrika ya Kusini bado inapiga hatua katika ukombozi wa kweli baada ya kuondoa ubaguzi wa rangi. Miaka 5 ya Nelson Mandela kama Rais inakuonyesha Madiba mwenye madaraka na namna aliyatumia kuanza kusuka jamii mpya. Suala la uteuzi wa mrithi wake ambalo limeendelea kuwa gumzo kwa miongo miwili nimeelezwa vizuri kwenye kitabu cha Dare not linger na baadhi ya maelezo yanafanana kidogo na maelezo ya kwenye kitabu cha Ramaphosa hapa. Ni kweli Mandela alimtaka Ramaphosa kuwa mrithi wake lakini alishauriwa tofauti na Rais mstaafu Kaunda na Rais mstaafu Nyerere kwamba Thabo Mbeki ndiye chaguo lao na Mandela akatii ushauri wa wenzake. Mambo ya sasa ya Afrika Kusini hasa kuhusu ufisadi na uongozi mbovu yanatia simanzi sana. Vitabu 5 vifuatavyo vinahusu Afrika Kusini na baadhi ya watu wake muhimu kwenye siasa za ukombozi na siasa za sasa.

18. Dare Not Linger: The Presidential Years
Nelson Mandela and Mandla Langa

19. A Simple Man: Kasrils and the Zuma enigma
Ronnie Kasrils

20. The President’s keepers: Those keeping Zuma in power and out of prison
Jacques Pauw

21. Ramaphosa: The Man who would be King
Ray Hartley

22. Woman in the wings: Nkosazana D Zuma and the race for the presidency
Carien du Plessis

Nimekuwa mfuatiliaji wa masuala ya mfumo wa kodi za kimataifa na namna baadhi ya nchi za visiwa zikiitwa Tax Havens zinavyotumika kuficha fedha chafu zinazotokana na ukwepaji wa kodi. Naheshimu kazi za waandishi wa habari za uchunguzi na Wabunge wenzangu katika kufichua namna dunia inaibiwa nan chi zinazoendelea kupoteza matrilioni ya fedha. Afrika peke yake inapoteza USD 50 bilioni kila mwaka kutokana na mfumo fyongo wa kodi za kimataifa. Vitabu hivi 2 vimenisaidia sana kuuelewa mfumo wa kodi za kimataifa na namna mabunge yanaweza kubomoa mfumo wa kinyonyaji unaonufaisha matajiri wachache.

23. The Panama Papers: Breaking the story of how the rich and powerful hide their money
Bastian Obermayer and Fredrik Obermaier

24. Called to Account: How corporate bad behavior and government waste combine to cost us millions
Margaret Hodge

Napenda historia ya Afrika. Sikuwa nimemwelewa vizuri zaidi Mfalme Haile Selasie kama anavyoelezwa na Asfa. Kitabu changu cha mwaka 2017 ni Zanzibar Uhuru maana kimeleeza miezi ya mwanzo ya Uhuru wa Zanzibar na Mapinduzi na maisha ya baadaye kwa namna ambayo inaeleweka na kuondoa kabisa propaganda tulizolishwa mashuleni kuhusu Uhuru wa Zanzibar na Mapinduzi.

25. King of Kings: The triumph and tragedy of Emperor Haile Selasie of Ethiopia
Asfa-Wossen Asserte

26. Zanzibar Uhuru: A Revolution, two women and the challenge of survival
Anne M Chappel

Ndugu yangu Rakesh Rajani alinitambulisha kwa mwandishi Coates na nimejikuta ninasoma kila kazi yake. Mjadala wa mahusiano ya watu weusi na nchi ya Marekani bado mbichi kabisa.

27. We were Eight Years in Power: An American tragedy
Ta-Nehisi Coates

28. Between the world and me
Ta-Nehisi Coates

Bado naendelea kujifunza namna nchi zinatoa watu wake kwenye dimbwi la umasikini. Vile vile kuna haja ya kuelewa upya kabisa mfumo wa uchumi tofauti na nadharia tunazosoma darasani. Vitabu hivi viwili vinaweza kukupa maarifa mapya kabisa namna uchumi unaweza kutumikia watu badala ya watu kutumikia uchumi.

29. How China escaped poverty trap
Yuen Yuen Ang

30. Doughnut Economics: Seven Ways to think like 21st-century Economist
Kate Raworth

Naendelea kujifunza namna miji inaendeshwa ili kupata maarifa ya kutekeleza katika Mji wa Kigoma Ujiji ambapo tunajitahidi kujenga Manispaa ya Kijamaa katika nchi ambayo zimetupilia mbali sera za kijamaa na ukombozi wa mtu wa chini kabisa.

31. View from the city hall: reflections on governing Cape Town
Patricia De Lille and Craig Kesson

32. Taken for a ride: grounding neo liberalism, precarious labour, public transport in an African Metropolis
Matteo Rizzo

Nimefurahi kusoma kazi za Ally Saleh na nimeendelea kusoma riwaya za magwiji. Ally Saleh amechangia kuelewa muktadha wa kizanzibari katika maandiko yake. Jumba Maro ambayo sijaiorodhesha hapa na la kuvunda zinaeleza maisha ya Wazanzibari na harakati zao kwa lugha nyepesi ya kifasihi. The Roaster Bar kinafurahisha na kufundisha kuhusu maisha ya vijana wanasheria kwenye vyuo hewa vya sheria na changamoto za mfumo wa uhamiaji na utoaji haki huko Marekani. Riwaya ni Therapy.

33. After the fire
Henning Mankell

34. Rogue Lawyer
John Grisham

35. The Roaster Bar
John Grisham

36. La Kuvunda
Ally Saleh

Nina maliza mwaka na vitabu 2, Zeitoun cha Dave Eggers kuhusu hadithi ya familia moja ilivyofanya kazi ya kupigwa mfano kuhusu kimbunga cha Katrina huko New Orleans Marekani. Kitabu cha Pili ni The Feast of the Goat cha Mario Vargos Llosa kuhusu udikteta wa Rafael Trujillo wa nchi ya Dominican Republic ulivyoleta vita ya wenyewe kwa wenyewe na umwagaji mkubwa wa damu za raia wasio na hatia.

Sikufikia idadi ya vitabu vya mwaka 2016 lakini nimeongeza maarifa hususan kwenye eneo la misingi ya itikadi ya Ujamaa. Haukuwa mwaka mbaya kwenye usomaji, nilipata muda wa kutosha ingawa kuna vitabu sikumaliza au sikuvianza kabisa. Nimetimiza miaka 5 sasa natoa orodha kila mwezi Disemba na kupitia kwayo nimevutia watu wengi kupenda kusoma. Mungu akitupa uhai nitaendelea kuwatajia vitabu vyangu kila mwaka na pia tunaweza kujadili baadhi yake kwa pamoja.
Nawatakia kheri ya mwaka mpya 2018 na mungu awasaidie kumaliza kwa amani mwaka 2017.

Zitto Kabwe, Mb

Kigoma Mjini

Kushoto: Mh. Zitto Kabwe na Mwandishi

Kulia: Abdilatif Abdalla na Juma Mwapachu wakiwa New Africa Hotel  katika
uzinduzi wa kitabu, ''Nyerere: The Early Years,'' kilichoandikwa na Thomas Molony
Abdilatif Abdalla na baadhi ya vitabu katika Maktaba yake nyumbani kwake Humburg

No comments: