Tuesday 2 January 2018

SHEIKH RAMADHANI ABBAS (1913 - 1983)


Sheikh Ramadhani Abbas

Sheikh Ramadhan ibn Abbass ibn Muhammed Ahmed Said Al Shirazy Rahimahullah (Mzee Baba), alizaliwa mwaka 1913, Magogoni, Kigamboni, Dar es Salaam. Alisoma Bagamoyo na Unguja mpaka Misri. Alisoma kwa Sheikh Omar Ally Hassan Al Mazrui, Sheikh Gombe aliezikwa makaburi ya Magomeni Dar es Salaam.

Akiwa Sheikh tayari mwalimu bado alikuwa hatosheki na ilmu, akapata pia kwa swaahib zake masheikh zake, maulamaa wenzake kama wakina Sheikh Amer Taju, Sheikh Hassan Bin Amir, Sheikh Mtumwa wa Nyuki, Sheikh Sulayman Alawi  Rahimahullah. Alianza kusomesha 1931 New Street (Mtaa wa Lumumba).

Alikuwa akipenda watu nao wakimpenda  kila rika, hakuwa tu mwalimu bali ni mlezi pia wa wanafunzi zake , jirani zake alikuwa mkarimu, mnyenyekevu, mcheshi mtu wa matani hajui kuchukia. Wanafunzi wake ni wengi, miongoni mwao Ni mwalimu wangu Sheikh Uwesu bin Mzee Kibosha (Mudir Madrasatil Khairiyyah), Sheikh Zubeir ibn Yahya Imamu Mkuu wa Msikiti wa Mtoro, Sheikh Hamid Jongo Imamu wa Msikiti wa Manyema, Sheikh Pongwa na wengine wengi.

Rafiki yake mkubwa Sheikh Qassim bin Juma Imam Msikiti wa Mtoro, Rahimahullah. Akiwapenda sana masharifu alikuwa kipenzi chake mkubwa na swaahib yake Shariff Hussein Badawy pamoja na Sayyid Ali Badawy Rahimahullah , na ndo mtu wa kwanza kwa Tanzania kupokea Maulidi ya Habshy (Suntum Durur) kutoka kwa Sayyid Ali Badawy na mpaka ile tareikh ya Maulid Riyadhwa, Lamu ndo ile ile tareikh ya huku kwetu Madrasatul Abbasiyyah, Alkhamisi ya mwisho wa Mfungo Sita.

Nanukuu kutoka kwa masheikh na masharifu zangu waliopokea hii, "Kwamba ukiyakosa maulidi ya Riyadhwa na ukajaaliwa kuyapata haya ya Abbasiyyah, au ukikosa Abbasiyyah ukapata ya Riyadhwa basi ni sawa (na hilo alilisema mwenyewe Sayyid Ali Badawy Rahimahullah.

Maulid Abbasiyya

Sheikh Ramadhan ibn Abbas alifariki tarehe 31 Januari 1983 sawa na Mfungo Saba tarehe 16 saa tano usiku Hospitali ya Aga Khan.

Rabbi awarahamu wanazuoni wetu wote waliotutangulia mbele ya Haqq.
Allahumma Aamiin.

Sheikh Abbas Ramadhani Abbas
Mudir wa Madras Abbassiya


No comments: